MGOMO WENYE MADUKA WAZIDI KUSAMBAA

Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum.
Mgomo wa wafanyabiashara wa mduka umesambaa mikoa kadhaa nchini kupinga matumizi ya mashine za kielektroniki (EFDs).
 
Mgomo huo ulioanzia kwa wafanyabiashara wa maduka Kariakoo, jijini Dar es Salaam kuanzia juzi, kupinga Mwenyekiti wao Johnson Minja, kukamatwa na polisi, sasa umesambaa hadi miji ya Mwanza, Iringa, Songea na Dodoma.
 
APANDISHWA KIZIMBANI
Minja (34), jana alipandishwa kizimbani katika Mahakama ya Mkoa wa Dodoma kwa makosa mawili likiwamo la kuzuia ukusanyaji wa kodi kwa kutumia EFDs na kusomewa mashitaka hayo mbele ya Hakimu Mkazi, Rebbeka Mbiru.
 
Wakili wa Serikali, Godfrey Wambari, alidai kuwa Septemba 6, mwaka 2014, katika ukumbi wa Chuo Cha Mipango Dodoma alitenda kosa la kushawishi wafanyabiashara kutenda kosa la jinai kwamba wasilipe kodi.
 
Katika shitaka la pili, siku na mahali pa tukio la kwanza mshtakiwa anadaiwa kuzuia ukusanyaji wa Kodi kwa kutumia mashine za EFD.
Upande wa Jamhuri haukuwa na pingamizi la dhamana.
 
Mshtakiwa alikana mashitaka yake.
 
Hakimu Mbiru alisema mshtakiwa atakuwa nje kwa dhamana kwa kuwa na wadhamini wawili akiwemo mtumishi wa serikali mmoja, watakaosaini hati ya dhamana ya Sh. milioni nne.
 
Wakili wa utetezi, Godfrey Wasonga, alidai kuwa mshtakiwa ni mfanyabiashara maarufu nchini na kwamba anaaminika hawezi kutoroka mahakama ipunguze masharti ya dhamana.
 
Hata hivyo, mshtakiwa alitimiza masharti ya dhamana na kesi hiyo itatajwa Februari 11, mwaka huu.
 
IRINGA
Katika hatua nyingine, wakazi wa mkoa wa Iringa jana walishindwa kupata huduma  muhimu kutokana na wafanyabiashara wenye maduka kuungana na wafanyabiashara wa mikoa mingine katika mgomo wa kufungua maduka baada ya Minja kukamatwa.
 
Mgomo huo umedumu kwa siku nzima na kusababisha wakazi wa manispaa ya hiyo kukosa huduma muhimu za kijamii.
 
Mwenyekiti wa wafanyabiashara mkoa wa Iringa, Odilo Nambanga, alisema kwamba mgomo huo wameungana na wenzao nchi nzima kufunga biashara zao mpaka matatizo yao ya msingi yatakapotatuliwa.
 
Nambanga alisema kauli mbiu yao ni mwenyekiti kwanza na masuala mengine yatafuata ikiwa ni pamoja na kuungana kwa umoja wao na kutatua matatizo yao.
 
Naye mfanyabiashara Sylivester Mmasi, alisema hawawezi kufungua biashara hata zipite wiki mbili hadi watakapopata tamko la kukamatwa mwenyekiti wao.
 
Alisema umesababisha wanafunzi kukosa huduma za vifaa vya shule hasa wale wanaokwenda shule zilizopo nje ya Manispaa ya Iringa na kulazimika kuhudhuria masomo.
 
SONGEA
Wafanyabiashara wa Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma wamelazimika kufunga maduka yao kupinga kitendo cha kukamatwa kwa Minja na kwamba mgomo huo utadumu mpaka hapo watakapopata uhakika wa usalama wake na si vinginevyo.
 
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo Tawi la Ruvuma, Isaya Mwilamba, alisema wamefunga maduka kusubiri hatma ya Minja.
 
Mwilamba alisema kuwa wafanyabiashara wote nchini wanasitisha shughuli zote hadi watakapojua hatma ya kiongozi na mtetezi wao.
 
 “Tunaitaka serikali kuzingatia nia njema ya kuundwa kwa kamati hiyo ya majadiliano na itoe taarifa stahiki kwa wafanyabiashara kwani tunapata wasiwasi kuwa kukamatwa kwake kiongozi wetu kunatokana na juhudi za wafanyabiashara kupinga ongezeko la kodi kwa asilimia 100 na matumizi ya mashine za EFD,” alisema Mwilamba.
 
Alisema serikali inapaswa kutumia njia za kidemokrasia kumaliza changamoto zake na siyo kutumia nguvu kuzima madai ya msingi ya wafanyabiashara hivyo ni vyema ikasikiliza kilio cha wafanyabiashara ambao kimsingi ndio wachangiaji wakubwa wa kodi za serikali.
 
MWANZA
 Baadhi ya wafanyabiashara wa maduka jijini Mwanza wa mitaa ya Lumumba, Pamba na Rwegosore, wamefunga maduka kupinga kukamatwa kwa Minja.
 
Akizungumza na NIPASHE jana, Michael Massanja, mfanyabiashara wa jijini hapa, alisema wamesikitishwa kukamatwa kwa kiongozi wao na wameamua kuungana kwa kufunga maduka kama walivyofanya wenzao wa Dar es Salaam.
 
Massanja alisema kukamatwa kwa kiongozi wao sio suluhisho la kuwafanya wafanyabiashara kutumia mashine hizo badala yake serikali izungumze na wafanyabiashara  husika ili kutatua mgogoro huo.
 
”Hatutafungua maduka yetu hadi pale tutakapopata taarifa ya Mwenyekiti wetu mahali alipo ingawa tumesikia yupo Dodoma,  lakini hatuna uhakika na hilo,” alisema Massanja.
 
Naye Zuberi Issa, mfanyabiashara wa maduka mtaa wa Pamba, alisema kufuatia kukamatwa kwa Mwenyekiti wao Minja, kumesababisha kutofanyika biashara yoyote kwa siku nzima ya jana, huku akisisitiza maduka kutofunguliwa.
 
”Tukio hili limechangia tusifanye biashara toka asubuhi kwa kuwa tumesisitiziwa na wenzetu kuungana ili tujue hatma ya kiongozi wetu yupo wapi na atapatikana lini,” alisema Issa.
 
Hata hivyo, Mwenyekiti wa wafanyabiashara Mkoa wa Mwanza, Christopher Wambura, hakupatikana kuzungumzia mgomo huo.
 
KARIAKOO BADO
Wafanyabiashara wa Soko Kuu Kariakoo Mtaa wa Kongo, jijini Dar es Salaam, wameendelea kugoma kufunga maduka yao kushinikiza kuachiwa kwa Minja.
 
Uchunguzi  uliofanywa na NIPASHE ulibaini kuwa karibu mitaa yote inayopatikana Karikoo, maduka mengi yalikuwa yamefungwa jana huku machache yakiwa yamefunguliwa.
 
Katika Mtaa wa Kongo, wafanyabiashara walikutwa wakiwa nje, hali iliyowawia vigumu wateja kupata mahitaji kama vile bidhaa kadhaa.
 
NIPASHE lilibaini baadhi ya maduka ya simu machache yaliyokuwa yamefunguliwa milango nusu hali iliyowafanya wateja kununua bidhaa za hizo kwa taabu.
 
Walipohojiwa wafanyabiashara hao kwa masharti ya kutotajwa majina yao, walisema wataendelea kugoma kufungua maduka yao hadi watakapojua sababu ya kukamatwa kwa kiongozi wao.
 
“ Hatufungui maduka yetu mpaka tujue sababu ya kukamatwa kwa Minja, tutayafungua endapo tutaelezwa sababu za kukamatwa kwake,” alisema mmoja wa wafanyabiashara hao.
 
Minja alikamatwa juzi  na Jeshi la Polisi na kusafirishwa kupelekwa mjini Dodoma kujibu mashitaka ya kuhamasisha wafanyabiashara wa mkoa huo wagome kufungua maduka kupinga matumizi ya EFDs.
 
Imeandikwa na Daniel Mkate, Mwanza, Peter Mkwavila, Dodoma; Gideon Mwakanosya, Songea; George Tarimo, Iringa na Hussein Ndubikole, Dar.
 
CHANZO: NIPASHE

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

WATU WAWILI WAMEFARIKI DUNIA NA WAWILI KUJERUHIWA KATIKA MATUKIO MAWILI TOFAUTI

 
Mawili tofauti ambapo katika tukio la kwanza maria hauule  mkazi wa Kijiji cha muhukuru songea vijijini mkoani ruvuma  ameuawa kwa kukatwa na shoka kichwani  na mume wake itwaye  salvatory ndimbo  na kasha mwili wake  kuutupa mto mkurumo.
Hayo yamesemwa na kamanda wa polisi wa mkoa wa ruvuma ACP Mihayo Msikhela Kamanda mihayo anasema chanzo cha  mauaji hayo ni ugomvi  wa kimapenzi ambapo marehemu maria haule mwenye miaka arobaini  alikuwa na uhusiano wa kimapenzi  na mwanaume mwingine aitwaye  anzekula na kutaka kuachana na  mumewe  salvatory ndimbo mwenye miaka sitini.
Jeshi la polisi linaendelea kumsaka mume wa  marehemu maria Bw. Ndimbo mbaye ametoroka baada ya kufanya unyama huo.
Katika tukio jingine kamanda mihayo amesema kuwa mwendesha bodabodan aitwaye haridi alifa amefariki dunia na watu wawili kujeruhiwa baada ya kugongwa na gari  yenye namba T934BTE,Toyota Mark TU lililokuwa likiendeshwa na mweka hazina wa CCM mkoa wa ruvuma Bw. Silimu Mohamed mbaye anashikiliwa na polisi.
 Chanzo:ITV Tanzania
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
KUELEKEA UCHAGUZI 2015: JE UNAPENDA NANI AWE KIONGOZI WAKO? JAZA FOMU HII FUPI HAPA

JANUARY MAKAMBA: NCHI IKO NJIAPANDA

Mbunge wa Bumbuli na pia ni Naibu Waziri wa Sayansi, Teknolojia na Mawasiliano, January Makamba.
 
Wakati Chama Cha Mapinduzi (CCM) kikijiandaa kupanga ratiba ya mchakato wa kuwapata wagombea wake ndani ya dola katika vikao vijavyo, Mbunge wa Bumbuli, January Makamba, ametahadharisha kwamba kama watapatikana viongozi ambao wamekuzwa na kuulea mfumo wa sasa uliopo, nchi isitegemee kupata mabadiliko yeyote ya maendeleo.
Makamba ambaye pia ni Naibu Waziri wa Sayansi, Teknolojia na Mawasiliano, ni miongoni mwa makada wa CCM ambao walishatangaza nia yao ya kutaka kuwania urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Makamba akihojiwa jana katika radio moja alisema hivi sasa nchi  ipo njia panda na mwaka 2015 ndio utakaoamua kati ya njia moja nchi kupaa kwa kuendelea kiuchumi au kuporomoka.

Alisema dalili za nchi kuwa njia panda ambazo zinaonekana ni pamoja na tatizo la vijana wengi kukosa ajira, mitafaruku, ukali wa maisha kuzidi kuongezeka miongoni mwa jamii na watu kuanza kuongea lugha za utengano.

Alisema kati ya njia hizo kuna mambo ambayo yanaweza kufanyika kuipaisha nchi au kuiporomosha na kwamba aina ya uongozi utakaopatikanani mwaka huu ndio utaamua hatma ya nchi.

“Naamini kwamba kwa zama hizi tulizokuwa sasa ambako kunahitaji mabadiliko makubwa sana katika mfumo wa siasa, mfumo wa utawala ,mfumo wa uongozi na mfumo wa uchumi na lazima kupata viongozi ambao hawakuwa sehemu ya kuuweka mfumo uliopo sasa,” alisema.

Aliongeza kuwa kama watapatikana  viongozi ambao wamekuzwa na kuulea mfumo uliopo sasa tusitegemea tutapata mabadiliko yeyote.

“Tunaamini kuwa vijana wameandaliwa vizuri, tukipata viongozi wa zama hizi ambao wamelelewa kiuongozi na wanaelewa uongozi na thamani ya zama tulizonazo sasa na wakaaminiwa nchi yetu itapaa kimaendeleo,” alisema.

Makamba alisema malalamiko ya wananchi yaliyopo yapo chini ya uwezo wetu kutegemeana aina ya kiongozi ambaye atapatikana ambaye atajali maslahi ya wananchi badala ya maslahi yake binafsi.

Makamba alisema Watanzania  wanapaswa kuondoa dhana kwamba nafasi ya juu ya urais ni lazima mtu uwe na uzoefu, na kwamba hadi sasa wenye uzoefu na suala la urais ni Mwalimu Julius Nyerere, Ali Hassan Mwinyi, Benjamin Mkapa na  Rais Jakaya Kikwete tu.

“Ukiacha hao marais wastaafu, hakuna mtu mwingine yeyote ambaye anaweza kusema kazi aliyoishika imemuandaa kuwa kiongozi mkubwa wa nchi kwa maana ya rais,” alisema.
 
CHANZO: NIPASHE
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

MBUNGE AKALIA KUTI KAVU MBINGA

Wafanyabiashara wilayani hapa, wametishia kutomchagua Mbunge wa Jimbo la Mbinga Mashariki, Gaudence Kayombo kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba kwa kile walichodai ameshindwa kuwatetea bungeni na badala yake ameunga mkono ongezeko la kodi la asilimia 100.
Wakizungumza wakati wa kikao cha wafanyabiashara na maofisa wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mbinga, mmoja wa wafanyabiashara hao, Benedict Lwena alisema wameumizwa na mbunge wao kushindwa kuwatetea kuhusu suala hilo. “Hatukumtuma bungeni kwenda kulala, bali kutuwakilisha, kutokana na kutugeuka nasi tumejipanga kumwangusha kwani hatuwezi kuwa na mbunge asiyejali kero za wananchi wake,” alisema Lwena.
Mfanyabiashara mwingine, Ally Mbunda alisema kwa muda mrefu wamekuwa wakiomba kukutana na mbunge huyo ili waweze kuzungumzia kero zinazowasumbua lakini amekuwa akisema amebanwa na majukumu mengine.
Hata hivyo, akizungumza kwa simu jana, mbunge huyo alikiri kusikia malalamiko hayo lakini akashangazwa na taarifa hizo akisema, tangu kikao kilipomalizika hakuna viongozi wala wafanyabiashara waliomfuata kumweleza hatua zilizofikiwa juu ya kikao hicho.
Alisema anashangaa kwa nini malalamiko hayo yanatokea kipindi hiki cha kampeni, “Siyo wafanyabiashara peke yao wanaopiga kura, kwanza sheria inapitishwa na wabunge wote na inatumika nchi nzima hivyo sioni haja ya wao kuniadhibu.”
 Chanzo:Mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

HATMA KINA LOWASSA, MEMBE, SUMAYE, WASIRA, MAKAMBA, NGELEJA MWEZI UJAO

Katibu wa Halmashauri Kuu (Nec) ya CCM Taifa, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye.
 
Makada sita wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ‘waliohukumiwa’ kutumikia ‘kifungo’ cha kutogombea nafasi za uongozi ndani ya chama hicho kwa miezi 12, baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la kuanza kampeni za kusaka urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu kabla ya wakati, wanakabiliwa na hatari ya kuongezewa zaidi adhabu hiyo.
Makada hao ni pamoja na mawaziri wakuu wastaafu, Frederick Sumaye na Edward Lowassa; Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu), Stephen Wasira.

 Wengine ni Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja na Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Januari Makamba, ambao wote mbali ya ‘kuhukumiwa’ kutumikia adhabu hiyo, pia wako chini ya uangalizi wa chama.

 Uwezekano wa makada hao kuongezewa zaidi adhabu hiyo, ni moja ya maazimio yaliyopitishwa na Kamati Kuu ya CCM katika kikao chake kilichofanyika juzi mjini Unguja, chini ya uongozi wa Mwenyekiti wa Chama hicho, Rais Jakaya Kikwete.

 Kikao hicho kilichofanyika kwa zaidi ya saba, kilijadili mambo matatu ya msingi, ikiwamo kuhusu adhabu dhidi ya makada hao, maadili ya chama na kashfa ya kampuni ya kufua umeme ya Independent Power Tanzania Limited  (IPTL) ya uchotwaji wa zaidi ya Sh. bilioni 300 katika akaunti ya Tegeta Escrow, iliyokuwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Azimio hilo lilitangazwa jana na Katibu wa Halmashauri Kuu (Nec) ya CCM Taifa, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, baada ya kumalizika kwa kikao cha Kamati Kuu ya Nec jana.

Nape alisema baada ya muda kwisha, itafanyika tathmini kuona kama walizingatia masharti ya adhabu zao au la.

“Na kama kuna, ambao watakutwa hawakuzingatia masharti ya adhabu zao wataongezewa adhabu,” alisema Nape.

Alisema chama hicho kitajadili mwenendo wao na kupitisha maazimio baada ya adhabu yao kumalizika mapema mwezi ujao.

Makada hao waliwahi kuitwa na Kamati Ndogo ya Nidhamu iliyokuwa ikiongozwa na Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara, Philip Mangula na kuwahoji.

Baada ya mahojiano hayo, Februari, mwaka jana, Kamati Kuu ya CCM ilitangaza uamuzi huo mzito dhidi yao.

KUHUSU ESCROW
Kuhusu uchotwaji wa fedha hizo katika akaunti hiyo, kamati kuu imeiagiza kamati hiyo ndogo ya maadili kuchukua hatua za kimaadili kwa wale wote waliohusika na ukiukwaji wa maadili katika kashfa hiyo.

Nape alisema vikao vya kuwajadili waliohusika katika kashfa hiyo vitaanza rasmi Jumatatu ijayo.

Alisema tayari barua zimeshapelekwa kwa wahusika katika kashfa hiyo kuwataka wafike kwenye kikao hicho.

Nape alisema CCM imesikitishwa na kashfa hiyo jinsi ilivyowahusisha wanachama wake waandamizi.

Kutokana na hali hiyo, alisema CCM inaunga mkono maazimio yote yaliyopitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania dhidi ya wote waliohusika na kashfa hiyo.

“Kamati kuu imejadili na kuamua waliohusika na sakata hilo kuwaondoa katika vikao vya maamuzi,” alisema Nape.

Hivyo, akasema kamati kuu imeitaka serikali na vyombo vinavyohusika kuendelea kutekeleza maazimio ya Bunge juu ya suala hilo baada ya kuanza kuyatekeleza.

 Pia iliwataka wote wanaopewa dhamana kujenga utamaduni wa kuwajibika, vinginevyo waliowapa dhamana wachukue hatua za kuwawajibisha.

“Kamati Kuu ya CCM baada ya kukaa kujadili suala hili kwa muda mrefu na kwa kina, imesikitishwa sana na sakata hili. Na kamati imetoa maazimio hayo, ambayo kamati ndogo ya maadili itafanya kikao tarehe 19/01/2015 kwa ajili ya utekelezaji wa agizo hilo,” alisema Nape.

 Mbali na hayo, alisema Kamati Kuu pia ilipitisha ratiba ya shughuli mbalimbali za kamati kuu za chama kwa mwaka 2015.

 Pia walipanga ratiba ya mchakato wa kuwapata wagombea wa CCM ndani ya dola, ambao utapangwa na vikao vijavyo vya chama.

Akizumnguzia hali ya uchaguzi mkuu ujao, Nape alisema CCM imejipanga vizuri na kwamba, ina uhakika wa asilimia 100 kupata ushindi wa kishindo.

Alivishauri vyama vya upinzani kujipanga vyema ili navyo viambulie viti vichache ili kuimarisha demokrasia ya mfumo wa vyama vingi.

APINGA UTARATIBU WA CUF
Hata hivyo, alipinga vikali hatua ya Chama cha Wananchi (CUF) kuondoa utaratibu wa kura za maoni katika kuwatafuta wagombea katika uchaguzi mkuu.

 Alisema CUF imeonyesha nia yake ya kutozingatia misingi ya demokrasia ya kuwapa uhuru wananchi kuchagua kiongozi wanayemtaka katika hatua za awali.

“CCM kamwe hata siku moja hatutawatoa wagombea mfukoni. Tuna utaratibu wetu wa kura ya maoni, ambao tutaufuata ili kuwapa nafasi wanachama kumchagua kiongozi wanayemtaka,” alisema Nape.

Alisema CCM ni taasisi inayoendeshwa kwa misingi ya demokrasia na maamuzi ya walio wengi na siyo kama Chama cha Kuweka na Kukopa (Saccos) kama vilivyo vyama vya upinzani, ambavyo maamuzi hutolewa na mtu mmoja, ambaye ni kiongozi mkuu.

Alisema wapinzani wasahau kuwa ipo siku ccm itang’oka madarakani na badala yake itaendelea kushinda chaguzi na kuliongoza taifa la Tanzania.

“Kama Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, anasema CCM tujiandae kuondoa virago vyetu Ikulu, tunamwambia hayo ni maneno ya mfamaji, haachi kutapatapa. Na maneno kama hayo ameshazowea kuyasema mara nyingi tangu alivyofukuzwa CCM,” alisema Nape.

SOKO LA MAHINDI
Alisema kamati kuu pia ilijadili suala la soko la mahindi na kuiagiza serikali kuangalia upya mfumo unaotumiwa na Hifadhi ya Taifa ya Chakula (NFRA) katika ununuzi wa zao hilo.

Nape alisema utaratibu wa sasa, ambao kwa kiasi kikubwa unanufaisha zaidi mawakala badala ya wakulima moja kwa moja, unatakiwa ubadilishwe ili uwanufaishe zaidi wakulima.
CHANZO: NIPASHE
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

KUNA TOFAUTI YA MAABARA NA MAJENGO YA MAABARA

  Mwenyekiti wa Halimashauri ya Musoma vijijini ambae ni Diwani wa Kata ya Nyankanga Magina Magesa,  akikagua ujenzi wa maabara katika shule ya sekondari Bisumwa, juzi
Desemba 9 mwaka jana ndiyo ulikuwa mwisho wa utekelezaji wa agizo la Rais Jakaya Kikwete kuhusu ujenzi wa maabara katika shule za sekondari za Serikali nchi nzima.
Akiwa katika mikutano ya hadhara katika Wilaya za Lushoto na Kilindi mkoani Tanga Julai, Rais Kikwete aliagiza ifikapo Novemba 30 aone vyumba vya maabara vimekamilika. Kutoka Novemba 30 muda ukaongezwa hadi Desemba 9.
Utekelezaji wa ujenzi
Tayari kuna mikoa iliyotekeleza ujenzi huo kwa asilimia zaidi ya 90, mingine asilimia 50 na hata 30 kwa baadhi ya mikoa.
Mikoa iliyotekeleza agizo hilo na asilimia katika mabano ni Dar es Salaam (100), Mbeya (95.45), Njombe (95), Kigoma chini ya asilimia 40, Morogoro (60) na Ruvuma zaidi ya asilimia 92.
Katika maeneo mengi utekelezaji wa ujenzi huu umekumbwa na kadhia nyingi zikiwamo walimu kukatwa fedha kwa nguvu, wananchi kutishwa na hata baadhi ya watendaji kuvuliwa nyadhifa zao na wengine kukumbana na kipigo.
Mfano barua ya Septemba 15, mwaka 2014 kutoka Halmashauri ya Kongwa mjini Dodoma kwenda kwa waratibu wa elimu wa kata, iliwataka watendaji hao kuhakikisha wanakusanya fedha za michango kutoka kwa walimu.
Barua hiyo ilibainisha viwango vilivyotakiwa kutolewa ku ni Sh60,000 (waratibu elimu kata), Sh60,000 (walimu ngazi ya mshahara TGTS F-G), Sh30,000 (ngazi ya mshahara TGTS D-E) na Sh20,000 (TGTS B-C).
Mratibu wa Mtandao wa Elimu Tanzania (TenMet), Cathleen Sekwao, anasema huwezi kuwaeleza wananchi wachangie maabara wakati wanaona fedha zipo ila wanafaidi wachache.
“Watu wanachota pesa wanakula halafu unapofika wakati wa uboreshaji wa elimu wananchi wachangie, kweli hiyo Sh1.6 trilioni si ingetosha kujenga hizo maabara lakini je, waliokula wamechukuliwa hatua gani,” anasema na kuongeza:
“Fedha zipo na wananchi, walimu wanalia kuchangishwa, mifumo ya uongozi ni mibovu kwani ingekuwa imara rasilimali tulizonazo zinazopotea kwa wajanja kujinufaisha wao ndiyo inatufikisha hapa.’’
Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba katika mahojiano na gazeti hili Oktoba mwaka jana, alikaririwa akisema Serikali imekuwa ikipoteza zaidi ya Sh1.6 trilioni kwa mishahara hewa nchini kila mwaka.
“Ukisoma taarifa za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), utagundua zaidi ya Sh1.6 trilioni zinapotea kutokana na mishahara hewa, fedha inayotosha bajeti ya wizara,” alieleza Nchemba.
Kwa wadau wengi wa elimu, fedha anazotaja Mwigulu na nyinginezo zingeweza kutumika katika vipaumbele ikiwamo ujenzi huo wa maabara ambao sasa unaendeshwa kwa nguvu ya wananchi kupitia maagizo ya viongozi wa Serikali.
Fedha nyingine zinazoweza kutumika katika shughuli za maendeleo ni pamoja na zile zinazosamehewa katika misamaha ya kodi. Kwa mfano Bajeti ya Serikali ya mwaka 2013/14, inaonyesha kwa mwaka huo zaidi ya Sh1.6 trilioni zilipotea kupitia misamaha ya kodi.
Walimu wa Sayansi
Wakati hamasa ya sasa ikiwa ni ujenzi wa maabara, baadhi ya watu wanauliza kuna mikakati gani ya kuwapata wataalamu wa maabara hizo na hata vifaa husika?
Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Ezekiel Oluoch anasema katika masomo ya Fizikia, Kemia na Baiolojia kuna upungufu wa asilimia 50 ya walimu.
Anasema jumla ya shule za sekondari za kata nchi nzima ziko 3,500 na zote hazina maabara na kwa maabara za masomo ya sayansi inahitaji wataalamu wa maabara mmoja, hivyo kwa zote watahitajika watatu.
“Kwa idadi hiyo jumla ya wataalamu wa maabara 12,000 watahitajika…maabara zinatakiwa kuwa zimekamilika Novemba 30 mwaka huu je, walimu wa kuziendesha wanatoka wapi au tutakuwa na majengo tu ya maabara?’’ anasema.
Anaongeza: “Nilichokuwa nakiona mimi wakati Serikali inapanga kujenga maabara, ingepanga pia kuandaa walimu wa kutosha na wataalamu wa maabara hizo lakini sasa tujiandae kuwa na majengo ya maabara na si maabara kama wanavyodai.”
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Dk Romanus Dimoso anasema changamoto anayoitazama katika ujenzi wa maabara ni ndogo kuliko ujenzi huo utakapokamilika.
“Sitoshangaa kama nikiona au kusikia majengo hayo yamebadilishwa matumizi kwani gharama za ujenzi kama tunahangaika hivi itakuaje gharamza za vifaa vya kufundishia na kujifunza ambavyo ni kubwa kuliko ujenzi wenyewe?” anahoji.
“Walimu bado ni tatizo na hata waliopo hawakusoma kwa vitendo na walijikita kinadharia zaidi sasa unapotaka watumike katika maabara sijui itakuaje,” anaongeza kusema.
Kauli ya Wizara
Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, (Tamisemi) anayeshughulikia elimu, Kassimu Majaliwa anasema maabara zitakapokamilika watawasiliana na ofisi ya utumishi ili kuhakikisha wataalamu wanaajiriwa.
“Mbali na walimu pia tutafanya juhudi za kuwaajiri wataalamu wa maabara hizo ambao watakuwepo katika maabara hizo ili kurahisisha zoezi zima la utoaji wa huduma kwa wanafunzi,” anasema.
 Chanzo:Mwananchi

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

Watanzania Tuitunze Amani Ya Nchi Yetu


Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa