MBINGA YANUIA KUPUNGUZA AU KUONDOKANA NA UTEGEMEZI

Mbinga. Ifikapo 2050, Wilaya ya Mbinga ina shauku ya kujiona inapunguza au inaondokana kabisa na utegemezi kutoka Serikali Kuu linapokuja suala la utekelezaji wa bajeti yake.

Shauku hii ilioneshwa siku chache zilizopita wakati wa mkutano uliowaleta pamoja wadau mbalimbali kutoa maoni kuhusu Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2025-2050.  

Kwa mwaka huu wa fedha (2024/25) mchango wa mapato ya ndani ya Halmashauri ya Mji wa Mbinga ni asilimia 10.4 ya bajeti nzima ya Sh31.6 billion.

Tafsiri yake ni kuwa utegemezi kwa Serikali kuu ni asilimia 89.6.

Kwa upande wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga mapato ya ndani yanachangia asilimia 17.5 ya bajeti nzima ya Sh48.1 billion.

Hii inamaanisha kuwa utegemezi wake kwa Serikali kuu ni asilimia 82.5.

Mkuu wa Wilaya ya Mbinga Mhe. Kisare Matiku Makori alisema kuwa ufanisi katika ukusanyaji mapato ya ndani kwa Halmashauri za Mji wa Mbinga na Wilaya ya Mbinga utachochea utoaji huduma bora kwa wananchi.

“Lazima tuzitumie vizuri fursa tulizonazo kama tunataka kuongeza mapato yetu ya ndani,” alisema Mhe. Makori huku akitolea mfano wa madhari nzuri za Wilaya ya Mbinga jinsi zinavyoweza kuwa kivutio cha watalii.

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Mbinga Stuart Kuziwa alielezea haja ya kuendelea kutengeneza mazingira wezeshi ya biashara na uwekezaji ili kuvutia wawekezaji zaidi.

“Tunapaswa kuja na mikakati itakayowapa wananchi na wawekezaji ujasiri wa kuwekeza katika maeneo mbalimbali na hivyo kuongeza makusanyo ya Halmashauri,” alisema Bw. Kuziwa.



Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga Bw. Joseph Rwiza alisema kuna haja ya wao kupunguza utegemezi kutoka Serikali kuu.

“Kwetu sisi tunaona suluhisho la kupunguza utegemezi kutoka Serikali kuu ni kutengeneza mazingira rafiki ya kuwa na uchumi jumuishi,” alisema Bw. Rwiza.

Askofu wa Kanisa Katoliki Jimbo la Mbinga John Ndimbo alisema kama Mbinga inataka kusimama yenyewe lazima ihakikishe inatumia ipasavyo rasilimali zake asilia.

“Tunapaswa kutumia ipasavyo fursa tulizonazo kama tunataka tusiwe wategemezi kwa Serikali kuu,” alishauri Askofu Ndimbo.
 



WANANCHI MJI MBINGA WATAKIWA KUSHIRIKI MIRADI YA BOOST

Na Alex Nelson Malanga

Afisa Habari----Mji Mbinga

Mbinga. Wananchi wa Halmashauri ya Mji wa Mbinga wametakiwa kushiriki ipasavyo katika utekelezaji wa miradi ya BOOST yenye thamani ya Sh419.1 milioni kwa kutoa nguvu kazi.

Serikali kupitia mradi wa uboreshaji elimu ya awali na msingi (BOOST), imeipatia Mji Mbinga kiasi hicho cha fedha kwaajili ya ujenzi wa madarasa 15 na matundu 30 ya vyoo katika shule za msingi Beruma, Masumuni, Nazareth, Changarawe na Luhangai.

Akizungumza siku ya Ijumaa (Agosti 2) katika shule ya msingi Nazareth, Bw. Xavery Mwihava, Afisa Elimu Takwimu, Idara ya Elimu ya Awali na Msingi, Halmashauri ya Mji Mbinga, alisema kuwa nguvu za wananchi zitaokoa fedha ambazo zingetumika kuajiri vibarua.

Alisema badala ya kutafuta kibarua kufanya shughuli ndogo ndogo kama kusafisha eneo, kuchimba msingi, kusogeza maji na matofali, wananchi wanapaswa kufanya wenyewe ili pesa itakayookolewa isaidie shughuli nyingine za ujenzi.

“Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imetupatia pesa, shukrani yetu ni kwa sisi kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa miradi,” alisema Bw. Mwihava.

Bw. Mwihava aliye mwakilishi Afisa Elimu Awali na Msingi, Halmashauri ya Mji wa Mbinga, katika utambulisho wa miradi ya BOOST aliongeza: “Hii miradi ni yenu, hivyo mnapaswa kuonesha  uzalendo wa hali ya juu.|

Alisisitiza kuwa wananchi wanapaswa kushirikiana na walimu, kamati ya shule na uongozi wa Serikali ya mtaa ili miradi itekelezwe kwa ubora zaidi.

“Inatakiwa tuimbe wimbo mmoja, haitapendeza wananchi kuwaachia walimu, kamati ya shule au serikali ya mtaa peke yao, ” alisisitiza.

Miradi ya BOOST itakayotekelezwa mwaka huu wa fedha ni ujenzi wa madarasa manne na matundu sita ya vyoo Shule ya Msingi Changarawe (Sh106.2 milioni) na madarasa matatu na matundu sita ya vyoo Shule ya Msingi Nazareth (Sh82.2 milioni).

Miradi mingine ni ujenzi wa madarasa matatu na matundu sita ya vyoo Shule ya Msingi Masumuni (Sh82.2 milioni) na madarasa matatu na matundu sita ya vyoo Shule ya Msingi Beruma (Sh82.2 milioni).

Pia mradi mwingine utakaotekelezwa ni ule wa ujenzi wa madarasa mawili ya mfano ya elimu ya awali na matundu sita ya vyoo Shule ya Msingi Luhangai (Sh66.3 milioni).
 



 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa