Home » » TAKUKURU: WAANDISHI PIGENI VITA RUSHWA

TAKUKURU: WAANDISHI PIGENI VITA RUSHWA



Na Alex Nelson Malanga

Afisa Habari----Mji Mbinga

Mbinga. Kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika baadaye mwaka huu, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imewataka waandishi wa habari wa Wilaya ya Mbinga kuwa mstari wa mbele katika vita dhidi ya rushwa.

Akizungumza wakati wa kikao kazi na waandishi wa habari Jumatatu ya Julai 29, Mkuu wa TAKUKURU wilaya ya Mbinga Bw. Frederick Msae alisema waandishi wa habari wana jukumu la kuelimisha wananchi kuhusu haja ya kuchagua viongozi waadilifu.

“Waandishi wa habari mna uwezo wa kuwafikia wananchi kiurahisi. Tumieni vema kalamu zenu kuwaelimisha wananchi kuhusu haja ya kuchagua viongozi pasipo vitendo vyovyote vya rushwa,” alisema kamanda Msae.

Aliongeza: “Waandishi wa habari msipopiga kelele kuhusu rushwa wakati wa uchaguzi, wananchi watachagua viongozi ambao hawatakuwa na msaada wowote kwa jamii.”

Ni haja ya serikali kuona wananchi wanachagua viongozi ambao wataweza kuchanganua na kupambanua changamoto mbalimbali ambazo wanakumbana nazo katika jamii.

 “Viongozi wanaohitajika ni wale ambao watapatikana kwa njia ya haki na hivyo kuwa daraja kati ya wananchi na serikali katika mambo mbalimbali,” alisema Bw. Msae.

Bosi huyo wa TAKUKURU kwa ngazi ya wilaya alionya kuwa waandishi wa habari wasipokuwa mstari wa mbele katika kupiga vita rushwa, itaathiri imani ya hadhira yao.

Bw. Msae pia alieleza umuhimu wa waandishi wa habari kuwa wazalendo kwa nchi yao kwa kutoa taarifa za vitendo vya rushwa pindi vinapofanyika au vinapo pangwa kufanyika.

Hii, alieleza, itaisaidia TAKUKURU kuwashughulikia wahusika na hatimaye kuondoa vitendo vya rushwa katika wilaya ya Mbinga.

Pia, alisema waandishi wa habari kama kioo cha jamii, wanapaswa kuwa waadilifu kwa kutoa taarifa sahihi kwa umma pamoja na kuwanadi, pale inapobidi, wagombea wote pasipo upendeleo.

“Mnapaswa kutoa taarifa za wagombea wote bila upendeleo wowote na bila kupokea rushwa,” alihitimisha Bw. Msae.

 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa