Home » » NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA ORYX WAGAWA MITUNGI YA GESI 1,050

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA ORYX WAGAWA MITUNGI YA GESI 1,050



Na Alex Nelson Malanga


Afisa Habari----Mji Mbinga


Mbinga. Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Judith Kapinga kwa kushirikiana na Kampuni ya Gesi ya Oryx Tanzania jumanne (Julai 23) waligawa mitungi ya gesi 1,050 kwa wananchi wa Wilaya ya Mbinga, Mkoa wa Ruvuma.


Ugawaji wa mitungi hiyo yenye thamani ya Sh45 milioni unalenga kuunga mkono jitihada za Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia.



Kati ya mitungi ya gesi 1,050 iliyotolewa katika ukumbi wa One Pacific uliopo katika Halmashauri ya Mji wa Mbinga, Mkoani Ruvuma, kampuni ya Oryx ilitoa mitungi 700 na Mhe. Judith mitungi 350.


“Serikali kwa kushirikiana na wadau wa nishati safi ya kupikia imejidhatiti katika kuhakikisha tunaongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia,” alisema Mhe. Judith huku akiipongeza kampuni ya Oryx kwa mchango wake wa mitungi ya gesi 700.


Kupitia Mkakati wa Taifa wa matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia (2024-2034), Serikali imedhamiria kuongeza kaya za watanzania zinazotumia nishati safi ya kupikia kutoka asilimia 10 ya sasa mpaka asilimia 80 ifikapo mwaka 2034.


Ikiwa ni sehemu ya jitihada za  kuongeza matumizi ya nishati safi, mpaka sasa Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), imesambaza mitungi ya gesi ya ruzuku 83,500 yenye thamani ya Sh3.5 bilioni, kwa mujibu wa Naibu Waziri wa Nishati.



Kama hiyo haitoshi, aliongeza Mhe. Judith, mwaka huu wa fedha serikali imepanga kutoa mitungi 452,445 yenye thamani ya Sh10 bilioni.

“Lengo letu ni kupunguza gharama za nishati safi ya kupikia na kwa kufanya hivyo naamini tutachochea matumizi ya nishati hiyo,” alisema Mhe. Judith.


Agenda ya nishati safi ya kupikia ni muhimu sana kwa mustakabali wa maendeleo ya Taifa letu na kwa kutambua hilo Mhe. Rais Dkt. Samia amekua kinara katika kuhamasisha matumizi ya nishati hiyo.


Sifa hiyo ya Mhe. Rais haiishii Tanzania tuu, bali imevuka hadi mipaka ya nchi hii mwanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.


Hii inadhihirishwa na yeye kuzindua ‘programu’ ya nishati safi ya kupikia Afrika yenye lengo la kuleta mageuzi na kumkomboa mwanamke.


Uzinduzi huo ulifanywa mwishoni mwa mwaka jana huko Dubai, Falme za Kiarabu wakati wa Mkutano wa 28 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Mabadiliko ya Tabianchi (COP 28).


Mkurugenzi Mtendaji wa Oryx Bw. Araman Benoit alisema: “Tunataka jamii ya Tanzania iachane na nishati chafu ambayo sio mbaya kwa afya tuu, bali ni hatari kwa mazingira pia.”

 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa