Home » » Wananchi Ruvuma hawajui sheria za mazingira

Wananchi Ruvuma hawajui sheria za mazingira

Jitihada za Serikali  kutunza na kuendeleza vyanzo vya maji katika bonde la mto Ruvuma na pwani ya kusini ili kuboresha huduma 
ya maji huenda zikatatizwa na mgongano wa sheria na sera ya misitu, kilimo, ardhi na ile ya maji.

Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa habari hizi mkoani Ruvuma umebaini kuwa wananchi wanaoishi karibu na vyanzo vya maji hawaelewi sheria za uhifadhi ardhi na sera mbalimbali ikiwepo kilimo kwanza pamoja na ile  ya wizara ya maji inayozuia kuendesha shughuli za kibinadamu kwenye mabonde na  vyanzo vya maji.

Baadhi ya wakulima wa mbogamboga katika bonde la mto ruvuma,matogoro mjini Songea, wamesema wanashangazwa na 
baadhi ya viongozi kuzuia shughuli za kilimo katika bonde hilo wakati serikali  ikihimiza wakulima kujikita zaidi ktk kilimo cha umwagiliaji.

 Wamesisitiza kuwa sheria ya mazingira inayowabana kutokufanya shughuli zozote za kibinadamu ndani ya mita 60 ili kutunza vyanzo vya maji inakwamisha utekelezaji wa sera ya kilimo kwanza hatua ambayo wamedai itaongeza umasikini kwa jamii inayotegemea kilimo cha mabondeni.

 Ofisa uhusiano wa bonde la mto Ruvuma na pwani ya kusini bw.Dickson Maganga amesema ofisi yake inatambua changamoto ya mgongano wa sera na sheria katika kuhifadhi rasilimali ya maji  ndio maana wameanzisha mpango shirikishi wa kutunza na kuendeleza rasilimali hiyo  kwa kuunda jumuiya za watumia maji katika mitaa ili kusaidia kueneza elimu ya umuhimu wa utunzaji wa vyanzo na mabonde ya mito katika eneo hilo.

 Wakati serikali ikitekeleza miradi mbalimbali ya maji bado kumekuwepo na tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama katika maeneo mengi nchini  hali inayosababishwa na mabadilko ya tabia nchi pamoja na  shughuli za kiuchumi zinazofanyika katika vyanzo vya maji zikiwepo kilimo,uchomaji 
wa mkaa na matofali,ufugaji na upasuaji wa mbao.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa