Home » » Wadai kutonufaika na rasilimali za taifa

Wadai kutonufaika na rasilimali za taifa

WATU wenye ulemavu wilayani Namtumbo, Ruvuma wamedai rasilimali za taifa zinawanufaisha zaidi watu wasiokuwa na ulemavu  ukilinganisha na watu wenye ulemavu.
Walitoa madai hayo kwenye mafunzo yaliyotolewa na shirika lisilo la kiserikali la kuwaendeleza watu wenye ulemavu na yatima (SHIKUWATA) kwa ufadhili wa The Foundation For Civil Society yalifanyika wilayani  hapa.
SHIKUWATA imeendesha mafunzo ya siku tano kwa watu wenye ulemavu Kata ya Namtumbo yenye lengo la kuwajengea uwezo wa kujua sera ya maendeleo na huduma kwa watu wenye ulemavu.
Wakichangia mada kwa nyakati tofauti juzi, waliiomba serikali kuzingatia uwiano katika mgawanyo wa rasilimali za taifa, ajira, kupewa matibabu bure kama ilivyo kwa watu wasiokuwa na ulemavu.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mkurugenzi wa shirika hilo, Magreth Mapunda, aliwataka washiriki hao kufuatilia mafunzo hayo kikamilifu ili yaweze kuwasaidia kujua haki zao za msingi.
Aliwataka watu hao wenye ulemavu kuwa huru katika kuchangia kero na changamoto mbalimbali zinazowakabili kwenye mafunzo hayo, ili waweze kuzitafutia ufumbuzi kwa kushirikiana na serikali.
Mratibu wa shirika hilo, Laura Martin, alisema wameamua kuendesha mafunzo hayo katika Kata ya Hanga, Namtumbo, Msindo na Namabengo kwa ajili ya kuwawezesha kujua sera inayozungumzia kundi lao kwa lengo la kuelewa kama inatekelezwa baada ya kugundulika kuwepo kwa tabaka kubwa la kuwatenga na mgawanyo wa rasilimali za taifa.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa