Home » » Serikali kuendelea kuagiza dawa ili kuimarisha hali ya upatikanaji wa dawa nchini

Serikali kuendelea kuagiza dawa ili kuimarisha hali ya upatikanaji wa dawa nchini

 
Na. Lilian Lundo – MAELEZO

Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ikishirikiana na Bohari Kuu ya  Dawa (MSD) inaendelea kuagiza dawa ili kuhakikisha zinapatikana muda wote.

Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu wa wizara hiyo Dkt.  Mpoki Ulisubisya alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam wakati akitoa taarifa ya hali ya upatikanaji wa dawa nchini.

“Kumekuwepo na taarifa zisizo na ukweli zilizotolewa na taasisi isiyo ya kiserikali inayofuatilia masuala ya afya nchini kwamba MSD inaupungufu mkubwa wa dawa ambapo taarifa hiyo inasema kuwa kuna makopo 173 ya dawa za  paracetamol nchi nzima, taarifa ambazo hazina ukweli wowote” alifafanua Dkt. Ulisubisya

Aidha ameeleza kuwa MSD imepokea makopo 10,000 ya vidonge vya paracetamol na kusambazwa katika vituo vyote vya kutoa huduma za afya nchi nzima.

Vile vile alisema kuwa MSD imesaini mkataba na mtengenezaji wa ndani kwa ajili ya kutengeneza makopo 138,000 ya dawa za  paracetamol yenye ujazo wa vidonge 1,000 ambazo zitaanza kupokelewa wiki ya kwanza ya mwezi Octoba mwaka huu na kusambazwa katika vituo vinavyotoa huduma za Afya nchini.

Hata hivyo alibainisha kuwa antibiotics na dawa za kupunguza maumivu (Ciprofloxacin, Ceftriaxone, Diclofenac, Co-trimoxazole, Amoxycyline, Doxycycline na Metronidazole) ambapo zilikuwa zikihitajika zaidi zimeshapokelewa na MSD na kupelekwa katika kanda zote za MSD kwa ajili ya kusambazwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini.

Aliendelea kwa kusema kuwa, dawa za Miradi Msonge ambazo zinatibu na kuzuia magonjwa ya Malaria, UKIMWI, Kifua Kikuu, Ukoma, Kichaa cha Mbwa, Uzazi wa Mpango na chanjo mbalimbali zipo za kutosha kwenye Bohari.

Pia amesema kwa chanjo ambazo ziliripotiwa kutokuwepo zinatarajia kuwasili nchini kuanzia  Octoba 2, 2016, ambapo kwa wale waliotakiwa kupata chanjo hizo lakini hawakupata kutokana na ukosefu huo watataarifiwa ili kuweza kufika kwenye vituo vya afya na kupata chanjo hizo.

Akielezea juu ya hali ya upatikanaji wa dawa nchini Dkt. Ulisubisya alisema kuwa, kwa sasa upatikanaji wa dawa nchi ni asilimia 53 ambapo katika aina 135 za dawa muhimu, aina 71 za dawa hizo zinapatikana ghalani na nyingine zipo kwenye vituo vya kutolea huduma.

Dkt. Ulisubisya alisema kuwa hali ya upatikanaji wa dawa itaimarika zaidi Octoba mwaka huu ambapo Serikali inategemea kupokea kiasi kikubwa cha dawa pamoja na chanjo.
 
Mwisho
 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa