
Mkuu wa Wilaya ya Songea, Polole Mgema
 
  WILAYA ya Songea mkoani Ruvuma inakabiliwa na tishio la kugeuka 
jangwa kutokana na wananchi kukata miti, kuchoma misitu moto na baadhi 
ya watumishi wasiokuwa waadilifu kuruhusu wafugaji kutoka mikoa 
mbalimbali nchini kuingiza idadi kubwa ya mifugo bila kufuata sheria.
 
Hayo yamesemwa na Mkuu wa Wilaya ya Songea, Polole Mgema wakati 
akitoa salamu za serikali katika kikao cha Baraza la Madiwani cha 
Halmashauri ya Wilaya ya Songea kilichofanyika katika Kijiji cha Lundusi
 katika Kata ya Maposeni.
“Kuna uharibifu mkubwa katika mlima Lihanje na nimekuwa nikitoa 
maagizo kwa watendaji wetu mara kwa mara kusitisha shughuli za kilimo 
katika mlima ule, hata hivyo bado imeonekana baadhi ya wananchi 
wanaendelea kukata miti na kufanya shughuli zao za kibinadamu,” alisema 
Mgema na kuongeza: “Kuna watumishi ambao ni wagumu sana kutekeleza 
maagizo ya serikali sasa mimi mwenyewe nitaanza operesheni ya kuwaondoa 
ndugu zenu, lakini msije kunilaumu kwa hatua nitakayochukua.”
Kwa mujibu wake, ataanza kupita kijiji hadi kijiji kwa ajili ya 
kuwatangazia wananchi kuhusu mpango wa serikali kutunza mlima Lihanje 
kutokana na umuhimu wake baada ya kuona watumishi waliopewa dhamana ya 
kusimamia uhifadhi wa mazingira katika mlima huo kushindwa kutimiza 
wajibu wao kwa sababu wanazozijua. Aidha, amewataka watumishi na 
madiwani kusimamia vema agizo la serikali la kutoruhusu uingizaji mifugo
 kutoka mikoa mingine na kuzuia biashara ya mkaa kwenda nje ya Wilaya ya
 Songea.
CHANZO HABARI LEO 
0 comments:
Post a Comment