Home » » Serikali yakipongeza Chuo cha St. Joseph

Serikali yakipongeza Chuo cha St. Joseph

WAZIRI wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Dk. Shukuru Kawambwa amekipongeza Chuo Kikuu cha Mtakatifu Joseph, tawi la Songea, mkoani Ruvuma, kwa kufundisha masomo ya sayansi kwa kuwa itapunguza uhaba wa wataalamu wa kada hiyo.
Dk. Kawambwa alisema hayo mjini hapa jana wakati wa mahafali ya nne ya chuo hicho yaliyohudhuriwa na viongozi wa vyama vya siasa, serikali, wazazi wa wahitimu na wananchi mbalimbali.
Alieleza kuwa anathamini mchango unaotolewa na chuo hicho kwa kuwa nchi yoyote haipati maendeleo bila wataalamu wa sayansi hivyo ameuomba uongozi wa chuo hicho kuongeza udahili wa wanafunzi hao.
Kwa upande wake mkuu wa chuo hicho Tanzania, Dk. Arul Raj, alimwomba waziri huyo kuangalia uwezekano wa serikali kutoa mikopo kwa wanafunzi wa stashahada badala ya mikopo hiyo kutolewa kwa wanafunzi wa shahada peke yake kwa vile baadhi yao wanashindwa kumudu gharama za masomo.
Naye Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Joseph Mkirikiti, aliwataka wazazi kuwahimiza vijana wao kujiunga na chuo hicho ili wapate ujuzi utakaowawezesha kujiajiri na kulifanya taifa lipige hatua ya maendeleo tofauti na ilivyo sasa.
Kwa upande wake mwenyekiti wa chuo hicho Askofu John Ndimbo wa Jimbo Katoliki Mbinga ameipongeza serikali kwa ushirikiano katika ufanisi wa chuo hicho kwa madai kwamba bila ya kupata ushirikiano huo wasingefanikiwa.
Katika mahafali ya chuo hicho kilichoanzishwa mwaka 2004 wahitimu 96 wa masomo ya sayansi ya kompyuta walitunukiwa vyeti.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa