Home » » KILWA YAAGIZA TANI 60 ZA CHAKULA CHA NJAA.

KILWA YAAGIZA TANI 60 ZA CHAKULA CHA NJAA.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

HALMASHAURI ya Wilaya Kilwa imeagiza tani 90 za mahindi mkoani Ruvuma kwa ajili ya kaya zilizoathiriwa na mafuriko.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kilwa, Twaib Mbasha aliyasema hayo alipozungumza na wajumbe wa Baraza la Madiwani lililofanyika jana.

Alisema halmashauri imechukua hatua mbalimbali kukabiliana na tatizo hilo.
“Gari liko njiani likitokea mkoani Ruvuma linalosafirisha mahindi kuletwa wilayani hapa,” alisema.
Mbasha alisema ni vigumu kuwaacha wananchi hivi hivi bila ya kutoa msaada kwao, kwani hawakutegemea kama wangepatwa na mafuriko.

Alisema juhudi nyingine zilizochukuliwa ni kuwasiliana na ofisi ya Mkuu wa Mkoa na Kitengo cha Maafa cha Ofisi ya Waziri Mkuu ili kupata vyakula, dawa na huduma nyinginezo wanazohitaji wananchi hao.
Madiwani walisema hali si nzuri kwa kata zote, zilizopata mafuriko mwezi uliopita, kwani zinahitaji chakula na kuna hatari ya kutokea magonjwa ya milupuko.

Diwani wa Nanjilinji, Ally Yusufu alisema ekari 3,875 za mashamba ziliathiriwa na mafuriko ya Januari 22 hadi 26 mwaka huu.
Mazao ya chakula yaliyoathiriwa kwenye ekari hizo ni ekari 1,675 za mahindi, 207 mpunga, ekari 88 mtama, 144.5 muhogo, 1755 ufuta na ekari tatu za migomba.

Alisema kaya zilizoathirika ni 771 zenye watu 3,084. Watu hao hawana mahala pa kuishi na sasa wanaishi kwa majirani, marafiki, ndugu na jamaa.
CHANZO: HABARI LEO.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa