Home » » WAKULIMA WA MAHINDI 'WAILILIA' SERIKALI

WAKULIMA WA MAHINDI 'WAILILIA' SERIKALI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
WAKULIMA wa mahindi wilayani Songea mkoa wa Ruvuma, wameiomba serikali kuongeza fedha kwa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) Kanda ya Songea ili wanunue mahindi mengi kwa msimu wa kilimo wa mwaka 2016/2017.
Wakulima hao walisema kutokana na hali ya hewa ya mwaka huu, hasa kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha kwa wingi katika maeneo mkoani Ruvuma, wana imani uzalishaji utakuwa mkubwa, ikilinganisha na msimu uliopita.
Walisema ni vyema sasa serikali ikaanza kutafuta fedha za kutosha kwa ajili ya maandalizi ya ununuzi wa mazao yao, kwa kuwa viongozi wa serikali wanapita kwa wakulima na kuwahamasisha waongeze juhudi, jambo lililoungwa mkono na wakulima wengi wa mkoa huo.
Mkazi wa kijiji cha Mlilayoyo, Joseph Ngonyani alisema wakulima wengi wameitikia mwito wa viongozi unaotaka kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara mashambani.
Hata hivyo, wasiwasi wao mkubwa ni kama serikali itanunua mazao yao hasa mahindi, zao ambalo ni tegemeo kubwa la kiuchumi.
Robet Mapunda wa kijiji cha Hanga alisema katika msimu wa 2013/2014 na 2015, wakulima wengi walilazimika kuuza mahindi yao kwa hasara kutokana na utaratibu uliotumika wa NFRA kuwatumia mawakala kwenda vijijini kununua mahindi kwa bei ndogo ya Sh 200 na wao kuizuia serikali kwa Sh 500 hadi 550 kwa kilo.
Aliongeza kuwa kutokana na utaratibu huo, hakuna mkulima aliyenufaika na kilimo, badala yake mawakala ndiyo walifaidika na kuwaacha wakulima wengi wakiwa masikini.
Mapunda alisema wakulima walilazimika kuuza kwa bei ya ‘kutupa’ kwa vile walishindwa kupata nafasi ya kupeleka moja kwa moja katika vituo vilivyowekwa na NFRA, kwani wachache ndiyo waliopata nafasi hiyo jambo lililowaumiza wakulima wa mahindi katika maeneo mbalimbali mkoani Ruvuma.
 CHANZO ; HABARI LEO.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa