Home » » ‘Acheni shughuli za binadamu kwenye vyanzo vya maji’

‘Acheni shughuli za binadamu kwenye vyanzo vya maji’

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 



MKURUGENZI Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga, Venance Mwamengo, amepiga marufuku shughuli zote za kibinadamu kufanyika kandokando ya vyanzo vya maji kupunguza tatizo la uhaba wa maji ambalo limekumba eneo kubwa la wilaya hiyo.
Aidha Mwamengo, amezuia pia shughuli za kibinadamu ikiwamo kilimo katika milima jirani ya chanzo na mradi wa maji katika kijiji cha Kigonsera ambapo baadhi ya watu wamesababisha mradi wa maji katika kijiji hicho uliotumia kiasi kikubwa cha fedha kushindwa kufanya kazi.
Mwamengo alipiga marufuku shughuli hizo hivi karibuni wakati akizungumza na wananchi wa kijiji hicho na kuziagiza mamlaka zinazohusika kuhakikisha zinalinda vyanzo vyote vya maji kijijini hapo.
Pia aliwaagiza watendaji wa vijiji na kata, kuwasaka na kuwafikisha mahakamani watu wote waliosababisha mradi huo kushindwa kufanya kazi iliyokusudiwa licha ya serikali kutumia fedha nyingi kutekeleza mradi huo kuwaondolea wananchi kero hiyo ya muda mrefu.
Aliwataka watendaji hao, kuwashirikisha askari mgambo kufanya msako kabambe ambao utafanikisha kuwapata wahusika na pia kufanya doria ya mara kwa mara katika maeneo hayo muhimu kuzuia watu wachache wanaoharibu vyanzo hivyo.
“Kama watendaji mtashindwa kupata waharibifu hao wa vyanzo vya maji mimi mwenyewe kuanzia wiki ijayo nitaanza msako kuwatafuta watu ambao ni kikwazo katika mipango mingi ya maendeleo wilayani kwetu,” alisema Mwamengo.

Chanzo Gazeti la Habari Leo
 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa