Home » » Mbinga waukataa Mfuko wa Vidung’ata

Mbinga waukataa Mfuko wa Vidung’ata

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


HALMASHAURI ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma imeombwa kuufuta Mfuko wa Vidung’ata, unaohudumia wakulima wa kahawa wilayani humo.
Ombi hilo lilitolewa na wanachama wa Chama cha Ushirika wilayani Mbinga (MBIFACU).
Walisema hayo juzi katika mkutano wao kwa nyakati tofauti. Walisema mfuko huo umekuwa ukiwanufaisha baadhi ya watendaji waliopo serikalini na sio wakulima hao.
Kwamba makato ya fedha wanazokatwa katika kila msimu wa mavuno ya kahawa ni makubwa mno. Fedha hizo zililenga kununua dawa ya kuhudumia zao hilo, lakini cha kushangaza dawa hizo kwa ajili ya wakulima, zimekuwa haziwafikii. Lengo la kuunda Mfuko wa Vidung’ata ni kudhibiti wadudu wanaoshambulia mti wa kahawa, hasa katika kipindi cha masika.
Fedha wanazokatwa, Sh 50 kwa kila kilo moja ya kahawa mnadani Moshi, ilipaswa zikafanye kazi iliyolengwa na sio vinginevyo.
Walishauri waunde mfuko wa pembejeo za kilimo wao wenyewe na makato ya fedha zao, yaelekezwe huko; na si jambo hilo kushughulikiwa na watendaji wa serikali.
Mkulima wa kata ya Ngima, Wilson Kapinga, alisema wanaukataa mfuko huo kutokana na baadhi ya watendaji wa serikali, mabwana shamba, kukosa uaminifu wa kufikisha dawa kwa wakulima. Dawa hizo huishia mikononi mwao na kujinufaisha wao binafsi.
Kapinga alisema maofisa ugani hao, muda mwingi wamekuwa wakiishi mjini badala ya kuwa karibu na wakulima vijijini. Kitendo hicho kinawafanya washindwe kuwajibika ipasavyo, ikiwamo kuwafundisha wakulima utunzaji bora wa mazao yao shambani.
Mkulima mwingine wa kahawa, Peter Komba wa kata ya Myangayanga alisema umefika wakati watendaji hao wachukuliwe hatua za kinidhamu. Kwamba kutowajibika ipasavyo katika maeneo yao ya kazi, liwe fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo.
Mwenyekiti wa MBIFACU wilayani Mbinga, Stanley Lupogo aliunga mkono hoja hizo. Alitaka wakulima wa kahawa kuzalisha zao hilo kwa wingi na kwa ubora unaokubalika katika soko la ndani na nje ya nchi.

Chanzo Gazeti la Habari Leo
 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa