Home » » Aflatoxin yahatarisha afya za walaji

Aflatoxin yahatarisha afya za walaji

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.




UELEWA mdogo kuhusu aina ya sumu inayozalishwa na kuvu waishio kwenye udongo au mimea na nafaka zilizooza, umesababisha vita dhidi yake nchini kutofanikiwa ipasavyo hivyo kuhatarisha afya za walaji.
Katibu Mkuu, Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Dk Florens Turuka alisema sumu hiyo ijulikanayo kama aflatoxins, inasababisha usalama mdogo wa chakula na inahatarisha afya kwa walaji .
Akizungumza jijini Dar es Salaam kwenye mkutano uliozungumzia mapambano dhidi ya sumu hiyo , Turuka alisema sumu hiyo pia inaharibu biashara ya bidhaa za mazao hasa nafaka.
Pamoja na mambo mengine, wajumbe wa mkutano huo walijadili namna bora ya kuhusisha mapambano ya sumu hiyo kwenye miradi, programu na mipango mbalimbali.
Dk Turuka alisema, serikali itatoa kila aina ya ushirikiano kuhakikisha kuwa juhudi zote za mapambano dhidi ya aflatoxin zinafanikiwa. Kwa mujibu wa Turuka, aflatoxin ni tatizo kubwa kwenye mfumo wa chakula nchini hususan kwenye mahindi, karanga na maziwa.
“Vyakula hivi ni kati ya vinavyoliwa kwa wingi hapa nchini,” alisema.
Alisema bado juhudi kubwa zinatakiwa kufanywa kuondokana na tatizo hilo ambalo huweza kusababisha saratani ya ini. Utafiti wa hivi karibuni umeonesha kuwa maeneo ya ukanda wa Mashariki na Magharibi nchini ndiyo yaliyoathirika zaidi na sumu hiyo katika mfumo wa vyakula.
Alishukuru Kamisheni ya Umoja wa Afrika kwa juhudi zake za kudhibiti sumu hiyo.
Pia alishuruku timu ya wadau wanaopambana na sumu hiyo (Partnership for Aflatoxin Control in Africa -PACA) kwa kuratibu mkutano huo. Licha ya Tanzania ambaye ni mwenyeji, mkutano huo ulihudhuriwa na wajumbe kutoka Gambia, Malawi, Senegal na Uganda.


Chanzo Gazeti la Habari leo

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa