Home » » Bei ya kununua mahindi yaongezwa

Bei ya kununua mahindi yaongezwa

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
SERIKALI kupitia Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA), Kanda ya Songea, imelazimika kuongeza bei ya kununulia mahindi ya wakulima mkoani Ruvuma kutokana na ushindani mkubwa, baada ya kuwepo kwa wanunuzi binafsi wengi wanaonunua mahindi kwa bei kubwa.
Kutokana na ushindani uliopo, NFRA kuanzia Novemba 7, mwaka huu ililazimika kupandisha bei ya kununua mahindi hadi kufikia Sh 580 kwa maeneo ya vijijini na Sh 600 kwa watakaoleta katika kituo kikuu cha Ruhuwiko mjini Songea.
Hayo yalisemwa na Kaimu Meneja wa NFRA Kanda ya Songea, Majuto Chabruma, alipozungumzia kazi ya ununuzi wa mahindi katika vituo mbalimbali vilivyotengwa katika wilaya zote za mkoa wa Ruvuma.
Chabruma alisema mwaka huu Serikali ilituma Sh bilioni 6.4 kwa ajili ya kununua mahindi tani 12,000 za awali huku malengo ikiwa ni kununua tani 22,000 na bado wanaendelea na kazi hiyo japo hawajafikia lengo lao.
Hata hivyo, kuna ushindani mkubwa wa soko kutoka kwa watu na kampuni binafsi ambazo zimeingia mkoani Ruvuma kwa ajili ya kununua mahindi.
Chabruma alisema serikali imeona ni vyema kuongeza bei ya mahindi ili kukabiliana na ushindani wa bei iliyopo sokoni, jambo lililosababisha kupungua kwa mahindi.
Alisema bado wakala unaendelea kununua ziada ya mahindi ambayo bado ipo kwa wakulima na wauzaji wengine katika kituo cha Ruhuwiko Songea na amewashauri wakulima mkoani Ruvuma ambao bado wana mahindi nyumbani kuyauza kwa wakala huo.
Alisema hatua hiyo itaiwezesha serikali kufikia malengo yake na nchi kwa jumla iwe na akiba na kuwezesha kutoa nafaka hiyo pindi kutakapojitokeza uhaba wa chakula nchini.
Aidha, Chabruma aliwakumbusha wakulima mkoani Ruvuma kuanza maandalizi ya msimu mpya wa kilimo wakati huu kwani mvua za kwanza zimeshaanza kunyesha katika maeneo mbalimbali ya mkoa huo, pamoja na baadhi ya mikoa mingine nchini.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa