Home » » MHE. POSSI: JAMII IWASHIRIKISHE WATU WENYE ULEMAVU KATIKA FURSA ZOTE ZA MAENDELEO

MHE. POSSI: JAMII IWASHIRIKISHE WATU WENYE ULEMAVU KATIKA FURSA ZOTE ZA MAENDELEO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


Na.Mwandishi Wetu
Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Watu wenye Ulemavu, Mhe. Dkt. Abdallah Possi ameiasa jamii kuwashirikisha watu wenye ulemavu katika shughuli zote za maendeleo ili kusaidia kuwainua na kuondokana na dhana ya utegemezi na kuwakwamua kiuchumi.
Dkt.Possi ameyasema hayo wakati wa ziara yake katika Wilaya za Mbinga, Songea Vijijini na Nyasa mkoani Ruvuma ambapo alitembelea Shule zenye kuhudumia watu wenye mahitaji maalum za Songea Boys, Luhira, Huruma na Kituo cha Kulelea wenye ulewavu cha Peramiho Disabled Persons Action (PEDIPA) na Kituo cha kulele wazee na wenye ukoma cha Nge Wilayani Nyasa.
Katika ziara hiyo Mhe.Possi alibaini changamoto nyingi za watu wenye ulemavu na kuishauri jamii namna pekee ya kutatua changamoto wanazokabiliana nazo ni jamii kuona umuhimu wa kuwashirikisha watu hao katika mipango yote ya maendeleo.

“Halmashauri ziandae mipango ya kuwawezesha watu wenye ulemavu kuweza kushiriki kikamilifu katika kujitafutia kipato na hii itasaidia kuondokana na hali ya utegemezi na kuondoa mitazamo hasi juu ya watu wenye ulemavu kuwa hawawezi” .Alisema Mhe.Possi.

Waziri Possi alisisitiza kuwa ni lazima Halmashauri ziwe na ubunifu wa miradi ya maendeleo itakayo walenga watu wenye ulemavu, “Ni vyema sasa kuwe na jitihada za makusudi za kuunda miradi maalum kwa ajili ya kuwapa nafasi za ushiriki ili kujitafutia vipato na kuyakabili mazingira yao, ikumbukwe wakina mama waliachwa nyuma kwa muda mrefu ila baada ya kupaza sauti zao tunaona sasa wanasikika hivyo hivyo iwe kwa watu wenye ulemavu” Alisitiza Dkt.Possi.
Aidha Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Nyasa Dkt.Osca Albano alisisitiza kuyapokea maelekezo yote ya Naibu Waziri Mhe.Possi kwa vitendo na kumhakikishia kuwa Wilaya yao itakuwa mstari wa mbele katika kulitekeleza hilo.
 “Sisi tunafanya kazi kwa ushirikiano mzuri na Halmashauri hivyo ni vyema tukalichukua hilo kuangalia namna tunavyoweza kuliweka katika mipango yetu yote ya maendeleo ili kuwasaidia na kufikia lengo la serikali,” alisema Dkt. Albano.
Nae Katibu Tawala Wilaya ya Songea Bw. Edmund Siame aliomba halmashauri zote ziwe zinatoa mrejesho mapema juu ya maagizo yanayotolewa na viongozi wa juu huku Mwalimu Elswida Charles anayehudumia wanafunzi wenye mahitaji maalum akimweleza Dkt. Possi kuwa watu wenye ulemavu wanafarijika kutokana na jitihada anazofanya kuwainua watu wenye ulemavu.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa