Home » » RC: WATENDAJI WAZEMBE WAWAJIBISHWE

RC: WATENDAJI WAZEMBE WAWAJIBISHWE



na Julius Konala, Songea
MKUU wa Mkoa (RC) wa Ruvuma, Said Mwambungu, amewaagiza wakurugenzi wa halmashauri za wilaya na manispaa mkoani humo kuwawajibisha kwa kuwasimamisha kazi au kuwafukuza maofisa watendaji wa vijiji na kata wazembe ambao watashindwa kuwadhibiti watu wanaofanya uharibifu wa mazingira kwa kuchoma moto na kukata miti ovyo.
Mwambungu alitoa agizo hilo jana wakati akifungua kongamano la kuweka mikakati ya kudhibiti moto hatarishi kwenye maeneo ya misitu mkoani humo lililoandaliwa na kitengo cha Misitu Uenezi, Kanda ya Kusini.
Mkuu huyo wa Mkoa (RC), alisema maofisa watendaji hao wengi wao wamekuwa wakiwafumbia macho wananchi wanaojihusisha na uharibifu wa mazingira na kwamba vitendo hivyo vinahatarisha usalama wa viumbe hai na uoto wa asili ambao ni rasilimali ya taifa kwa vizazi vijavyo.
“Vitendo hivi vya uharibifu wa misitu vimekidhiri sana hasa katika tarafa ya Madaba kwa kazi ya kuendeleza biashara ya uchomaji wa mkaa kinyume na taratibu za uvunaji wa misitu hiyo kwa kuwa kasi ya ukataji misitu haiendani na upandaji miti,” alisema Mwambungu.
Aidha, aliwaonya mabwana miti kuacha tabia ya kukaa ofisini kwa lengo la kutoa vibali vya uvunaji wa misitu badala yake wazungukie vijijini kwa ajili kutoa elimu kwa wananchi juu ya utunzaji wa mazingira.
Kwa upande wake, Katibu Tawala Mkoa wa Ruvuma, Hassan Bendeyeko, akifunga kongamano hilo alisema katika kukabiliana na tatizo hilo ni vema kamati za mazingira katika kata na vijiji zikapewa nguvu ili kupunguza kasi ya uharibifu huo.
Chanzo: Tanzania Daima


0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa