Home » » UHABA WA DAWA WAITESA SONGEA

UHABA WA DAWA WAITESA SONGEA

na Stephano Mango
BAADHI ya wagonjwa wanaopata matibabu katika kituo cha afya cha Mjimwema kilichopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea, Mkoa wa Ruvuma, wamelalamikia uhaba mkubwa wa dawa kituoni hapo na kusema waganga wanawashauri kununua dawa katika maduka binafsi ambako zinauzwa kwa bei kubwa.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti jana, wagonjwa hao walisema kwa muda mrefu wamekuwa wakifika kituoni hapo kwa lengo la kutaka kupata matibabu, lakini badala yake wamekuwa wakipewa ushauri wa waganga na kuandikiwa dawa ambazo kwenye kituo hicho hazipo.
Mmoja wa wagonjwa hao, alisema kwa muda mrefu amekuwa akisumbuliwa na kidonda, lakini kila alipokwenda kwenye kituo hicho kwa ajili ya kusafisha alikuwa akishauriwa akanunue dawa kwenye maduka ya watu binafsi, kwani kituo hicho kina uhaba wa dawa kwa muda mrefu.
Mgonjwa mwingine, alisema alipofika katika kituo hicho akiwa anasumbuliwa na malaria, aliambiwa hakuna dawa na badala yake akaelekezwa akanunue kwenye maduka binafsi.
“Jambo la kushangaza hata Panadol nazo wanadai hawana. Tunaiomba serikali kupitia Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kuona umuhimu wa kuihimiza Bohari ya Dawa (MSD) kuhakikisha inasambaza dawa kwenye zahanati na vituo vya afya kwa wakati muafaka, ili kuokoa maisha ya Watanzania wengi,” alisema.
Kwa upande wake, Mganga Mfawidhi wa kituo hicho cha afya, Dk. Daniel Mtamakaya, alipohojiwa kuhusiana na malalamiko ya wagonjwa hao, alikiri kwa muda mrefu kituo chake hakijapokea dawa kutoka MSD, jambo ambalo amedai limekuwa likileta usumbufu mkubwa kwa wagonjwa.
Dk. Mtamakaya alisema wamekuwa wakilazimika kuwapa ushauri wa kitaalamu wagonjwa, lakini dawa ni lazima waende wakanunue kwenye maduka ya watu binafsi, kwani tangu Juni mwaka huu hawajapata dawa.
Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Songea, Nachoa Zacharia, alisema kuna tatizo kubwa la uhaba wa dawa kwenye zahanati zote za manispaa hiyo kikiwamo kituo cha afya cha Mjimwema.
Chanzo: Taaanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa