Home » » Adaiwa kumuua mwanawe kwa kumbamiza kwenye lami

Adaiwa kumuua mwanawe kwa kumbamiza kwenye lami

Mkazi  wa kijiji cha Madaba Wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, Onestory Mgaya (31), ametiwa mbaroni kwa tuhuma za kumuua mtoto wake mwenye umri wa miaka saba kwa kumbamiza  kwenye barabara ya lami.
Kamanda wa Polisi mkoani Ruvuma, Deusdedit Nsimenke, alimtaja mtoto aliyeuawa kuwa ni  Nesta Mgaya.

Kamanda Nsimenke alisema tukio hilo lilitokea Februari 9, mwaka huu saa 5:00 asubuhi katika kijiji cha Lilondo wilayani Songea.

Alifafanua kuwa inadaiwa kuwa siku ya tukio, mtuhumiwa huyo, mkewe, Blesila Mponda (30)  na mtoto wao Nesta, walitoka Madaba kwenda kijiji cha Lilondo kusalimia wazazi.

Hata hivyo, alisema wakiwa njiani kurudi nyumbani kwao,mkewe Blesila alibaini kuwa amesahau kadi ya kliniki ya mtoto wao na hivyo akalazimika kumuachia mumewe mtoto huyo ili yeye akaichukue kadi hiyo.

Lakini alisema mtuhumiwa huyo alianza kumbamiza mtoto kwenye barabara ya lami huku akiwa amemshika miguu na kichwa chini.

Hata hivyo, alisema wakati akiendelea kufanya ukatili huo, watu waliokuwa jirani walikwenda kutaka kumuokoa mtoto huyo lakini mtuhumiwa alikimbilia porini na kumuacha mtoto..

Alisema wasamaria wema walimkimbiza mtoto huyo katika Kituo cha Afya cha Madaba kwa matibabu.

Kamanda Nsimenke, alisema baadaye mtoto huyo alipelekwa katika Hospitali ya Mkoa ya Songea kwa matibabu zaidi lakini alifariki dunia siku iliyofuata.

Hata hivyo, Kamanda Nsimenke alisema mtuhumiwa huyo alikamatwa siku hiyo hiyo na anatarajiwa kupelekwa kupimwa akili yake kabla ya kufunguliwa mashitaka ya mauaji.
 
CHANZO: NIPASHE
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa