Home » » Polisi 14 nguvuni kwa kuiba mali ya Sh900 mil

Polisi 14 nguvuni kwa kuiba mali ya Sh900 mil

Polisi mkoani Ruvuma, wameingia katika kashfa, baada ya askari wake kutuhumiwa kuiba vitu vyenye thamani ya zaidi ya Sh900 milioni waliyokuwa wakivilinda. Vitu hivyo ni mali ya mkandarasi aliyefukuzwa katika mradi wa ujenzi wa Barabara ya Namtumbo hadi Tunduru.
Tayari polisi 14 wamesimamishwa kazi na wanasubiri kuvuliwa magwanda ili kufikishwa mahakamani. Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ruvuma, Deusdedit Nsimike, jana alithibitisha habari hizi kwa njia ya simu.
Alisema tukio hilo limelifedhehesha Jeshi la Polisi na kwamba taratibu za kuwafukuza kazi askari hao zinaendelea kabla ya kufikishwa katika vyombo vya sheria.
Mtoa habari wetu alisema kashfa hiyo iligundulika mwezi uliopita, lakini haikutangazwa kutokana na unyeti wake na kwamba suala hilo limeishtua Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Ruvuma.
Akifafanua zaidi alisema kwamba Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads), waliipatia polisi kazi ya kulinda mitambo, magari na vifaa mbalimbali vya Kampuni ya Progressive Hgleig JV ya India, baada ya kampuni hiyo kushindwa kazi na hatimaye kufukuzwa.
Alisema Serikali iliifukuza kampuni hiyo na kutoa agizo la kushikilia mali zake hadi itakapolipa fidia kwa hasara iliyoipata.
Mtoa habari ambaye jina lake linahifadhiwa alisema askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) Ruvuma, walipata zabuni ya kulinda mali hizo, lakini baadaye imegundulika kuibwa mali za mamilioni ya fedha.
Baadhi ya mali zilizoibwa ni pamoja na mafuta, matairi na vipuri vya magari. Meneja wa Tanroads mkoani Ruvuma, Abraham Kisimbo, alithibitisha habari hizo.
Alisema tukio hilo ni baya na kwamba anayeweza kulizungumzia zaidi ni na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ruvuma au Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa