Home » » WARIDHIA KOROSHO KUUZWA MFUMO WA STAKABADHI

WARIDHIA KOROSHO KUUZWA MFUMO WA STAKABADHI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

WADAU wa zao la korosho wilayani Tunduru, mkoani Ruvuma wameridhia kuuza korosho kupitia mfumo wa Stakabadhi ya mazao ghalani kuanzia msimu huu wa mwaka 2014/2015 zikiwa ni juhudi za kujiletea maendeleo tofauti na sasa ambapo wakulima hao wamekuwa wakipata hasara na kuwanufaisha wajanja wachache pindi wanapouza mazao yao kupitia mfumo wa soko holela.

Aidha wadau hao pia wamewapiga marufuku viongozi wa Vyama vya Msingi vya Wakulima wilayani humo kuendelea na utaratibu wa kwenda kukopa mikopo katika mabenki na kwenda kuwalipa fedha hizo kama malipo yao ya awali na kwamba hali hiyo pekee ndiyo itakayo saidia kuondoa manung'uniko kwa wakulima kulalamikia kuibiwa fedha zao.

Wajumbe hao waliendelea kubainisha kuwa fedha hizo za mikopo zimekuwa ni mzigo mkubwa kwa wakulima kutokana na kutakiwa kulipiwa riba kubwa ambazo hutozwa na mabenki hayo hali ambayo imekuwa ikiwafanya wakulima kushindwa kulipwa malipo yao ya pili na ya tatu baada ya fedha hizo kuishia kulipia riba za mikopo hiyo katika mabenki ambayo hukopwa na viongozi hao wa vyama vya ushirika, mambo ambayo yamekuwa yakileta ugumu kwa wakulima kuupenda mfumo huo wa stakabadhi ya mazao ghalani.

Tamko hilo lilifikiwa katika mkutano uliohusisha wadau wa korosho wa kujadili mfumo wa kisheria wa kuuza mazao yao kwa kutumia mfumo wa stakabadhi ya mazao ghalani.

Aidha katika kuhakikisha kuwa mfumo wa ununuzi wa mazao hayo kwa wakulima unafanikiwa, wakulima hao walikubali kutekeleza makubaliano ya kukusanya mazao yao katika maghala yaliyopo katika maeneo yao na kusubiri wanunuzi waende kununua hukohuko na kugawiwa fedha zao kulingana na idadi ya kilo alizozikabidhi.

Awali akitoa mada ya dhana ya bei dira na utekelezaji wake Mkurugenzi mkuu wa Bodi ya Korosho Tanzania, Bw.Mfaume Juma alisema kuwa mfumo huo ulianza kuhamasishwa msimu wa mavuno na mauzo ya korosho mwaka 2013/2014 na kuanza kutumika katika Mikoa ya Lindi, Mtwara na Pwani.

Alisema kuwa baadaye wilayani Tunduru mkoani Ruvuma msimu wa mwaka 2007/2008 na kwamba kabla ya hapo wanunuzi walikuwa wakinunua kupitia mfumo wa soko holela lakini wakiwa wananunua kupitia bei dira ambayo ilikuwa ikipangwa na Bodi ya Korosho Tanzania.

Bw.Juma aliendelea kufafanua kuwa pamoja na bodi hiyo kujipanga kusimamia utaratibu huo kwa uwazi kwa kuwashirikisha wawakilishi wa wakulima wakati wa kuuza korosho zao pia wameandaa mkakati maalumu na mazingira ya kusimamia uuzwaji wa korosho za Tunduru ikiwezekana hata kuhakikisha korosho hizo zinauzwa kwa utaratibu wa malipwani.

Alisema kuwa kwa tani 1 huuzwa hadi kwa dola za Marekani 1400, sawa na sh.2,240,000 tani moja sawa na kila kilo moja itauzwa kwa bei ya sh. 2,240 zikiwa ni juhudi za kumuondoa mtu wa kati yani Madalali na viongozi wa vyama vya ushirika mabavyo vimekuwa vikijinufaisha kupitia mgongo wa wakulima, Bw. Juma Aliendelea kueleza kuwa Kupitia mfumo huo wa stakabadhi ya mazao ghalani kazi za vyama vya msingi ni kukusanya mazao na kuyatunza katika maghala ya chama,kupanga madaraja,kufungasha katika magunia yenye uzito sahihi, kusafirisha korosho hadi sokoni, kusimamia mauzo wakati wa minada na kuwagawia wakulima fedha zao.

Alisema kwamba mtindo wa kukopa fedha katika mabenki haupo katika utekelezaji wa mfumo huo na kwamba viongozi wabadhirifu katika vyama vyao wawatoe wakati wa uchaguzi na kuwaweka madarakani viongozi waadilifu.

Akifafanua matumizi ya mfumo huo Mwenyekiti wa mfuko wa kuendeleza zao la korosho Tanzania, Bw.Athuman Nkinde alisema kuwa pamoja na mkakati huo wa kuwadhibiti walanguzi hao mfuko huo umetenga sh. bilioni 6 kwa ajili ya kujenga viwanda vitatu katika Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, Mtwara na Wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani.

Alisema katika mpango huo kila kiwanda kimetengewa sh. bilioni 2 zikiwa ni juhudi za serikali kukuza soko la ndani ili kuwainua wakulima na kuwawezesha kuuza mazao yaliyosindikwa na kwamba, mkutano huo umelenga kuwajengea uwezo na kufungua upeo kwa wakulima na kuwawezesha wakulima kupata faida na kuiwezesha halmashauri kupata ushuru mkubwa na kuifanya halmashauri yao kujitosheleza katika bajeti zake za matumizi ya ndani

Chanzo:MMjira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa