Home » » HATMA KINA LOWASSA, MEMBE, SUMAYE, WASIRA, MAKAMBA, NGELEJA MWEZI UJAO

HATMA KINA LOWASSA, MEMBE, SUMAYE, WASIRA, MAKAMBA, NGELEJA MWEZI UJAO

Katibu wa Halmashauri Kuu (Nec) ya CCM Taifa, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye.
 
Makada sita wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ‘waliohukumiwa’ kutumikia ‘kifungo’ cha kutogombea nafasi za uongozi ndani ya chama hicho kwa miezi 12, baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la kuanza kampeni za kusaka urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu kabla ya wakati, wanakabiliwa na hatari ya kuongezewa zaidi adhabu hiyo.
Makada hao ni pamoja na mawaziri wakuu wastaafu, Frederick Sumaye na Edward Lowassa; Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu), Stephen Wasira.

 Wengine ni Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja na Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Januari Makamba, ambao wote mbali ya ‘kuhukumiwa’ kutumikia adhabu hiyo, pia wako chini ya uangalizi wa chama.

 Uwezekano wa makada hao kuongezewa zaidi adhabu hiyo, ni moja ya maazimio yaliyopitishwa na Kamati Kuu ya CCM katika kikao chake kilichofanyika juzi mjini Unguja, chini ya uongozi wa Mwenyekiti wa Chama hicho, Rais Jakaya Kikwete.

 Kikao hicho kilichofanyika kwa zaidi ya saba, kilijadili mambo matatu ya msingi, ikiwamo kuhusu adhabu dhidi ya makada hao, maadili ya chama na kashfa ya kampuni ya kufua umeme ya Independent Power Tanzania Limited  (IPTL) ya uchotwaji wa zaidi ya Sh. bilioni 300 katika akaunti ya Tegeta Escrow, iliyokuwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Azimio hilo lilitangazwa jana na Katibu wa Halmashauri Kuu (Nec) ya CCM Taifa, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, baada ya kumalizika kwa kikao cha Kamati Kuu ya Nec jana.

Nape alisema baada ya muda kwisha, itafanyika tathmini kuona kama walizingatia masharti ya adhabu zao au la.

“Na kama kuna, ambao watakutwa hawakuzingatia masharti ya adhabu zao wataongezewa adhabu,” alisema Nape.

Alisema chama hicho kitajadili mwenendo wao na kupitisha maazimio baada ya adhabu yao kumalizika mapema mwezi ujao.

Makada hao waliwahi kuitwa na Kamati Ndogo ya Nidhamu iliyokuwa ikiongozwa na Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara, Philip Mangula na kuwahoji.

Baada ya mahojiano hayo, Februari, mwaka jana, Kamati Kuu ya CCM ilitangaza uamuzi huo mzito dhidi yao.

KUHUSU ESCROW
Kuhusu uchotwaji wa fedha hizo katika akaunti hiyo, kamati kuu imeiagiza kamati hiyo ndogo ya maadili kuchukua hatua za kimaadili kwa wale wote waliohusika na ukiukwaji wa maadili katika kashfa hiyo.

Nape alisema vikao vya kuwajadili waliohusika katika kashfa hiyo vitaanza rasmi Jumatatu ijayo.

Alisema tayari barua zimeshapelekwa kwa wahusika katika kashfa hiyo kuwataka wafike kwenye kikao hicho.

Nape alisema CCM imesikitishwa na kashfa hiyo jinsi ilivyowahusisha wanachama wake waandamizi.

Kutokana na hali hiyo, alisema CCM inaunga mkono maazimio yote yaliyopitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania dhidi ya wote waliohusika na kashfa hiyo.

“Kamati kuu imejadili na kuamua waliohusika na sakata hilo kuwaondoa katika vikao vya maamuzi,” alisema Nape.

Hivyo, akasema kamati kuu imeitaka serikali na vyombo vinavyohusika kuendelea kutekeleza maazimio ya Bunge juu ya suala hilo baada ya kuanza kuyatekeleza.

 Pia iliwataka wote wanaopewa dhamana kujenga utamaduni wa kuwajibika, vinginevyo waliowapa dhamana wachukue hatua za kuwawajibisha.

“Kamati Kuu ya CCM baada ya kukaa kujadili suala hili kwa muda mrefu na kwa kina, imesikitishwa sana na sakata hili. Na kamati imetoa maazimio hayo, ambayo kamati ndogo ya maadili itafanya kikao tarehe 19/01/2015 kwa ajili ya utekelezaji wa agizo hilo,” alisema Nape.

 Mbali na hayo, alisema Kamati Kuu pia ilipitisha ratiba ya shughuli mbalimbali za kamati kuu za chama kwa mwaka 2015.

 Pia walipanga ratiba ya mchakato wa kuwapata wagombea wa CCM ndani ya dola, ambao utapangwa na vikao vijavyo vya chama.

Akizumnguzia hali ya uchaguzi mkuu ujao, Nape alisema CCM imejipanga vizuri na kwamba, ina uhakika wa asilimia 100 kupata ushindi wa kishindo.

Alivishauri vyama vya upinzani kujipanga vyema ili navyo viambulie viti vichache ili kuimarisha demokrasia ya mfumo wa vyama vingi.

APINGA UTARATIBU WA CUF
Hata hivyo, alipinga vikali hatua ya Chama cha Wananchi (CUF) kuondoa utaratibu wa kura za maoni katika kuwatafuta wagombea katika uchaguzi mkuu.

 Alisema CUF imeonyesha nia yake ya kutozingatia misingi ya demokrasia ya kuwapa uhuru wananchi kuchagua kiongozi wanayemtaka katika hatua za awali.

“CCM kamwe hata siku moja hatutawatoa wagombea mfukoni. Tuna utaratibu wetu wa kura ya maoni, ambao tutaufuata ili kuwapa nafasi wanachama kumchagua kiongozi wanayemtaka,” alisema Nape.

Alisema CCM ni taasisi inayoendeshwa kwa misingi ya demokrasia na maamuzi ya walio wengi na siyo kama Chama cha Kuweka na Kukopa (Saccos) kama vilivyo vyama vya upinzani, ambavyo maamuzi hutolewa na mtu mmoja, ambaye ni kiongozi mkuu.

Alisema wapinzani wasahau kuwa ipo siku ccm itang’oka madarakani na badala yake itaendelea kushinda chaguzi na kuliongoza taifa la Tanzania.

“Kama Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, anasema CCM tujiandae kuondoa virago vyetu Ikulu, tunamwambia hayo ni maneno ya mfamaji, haachi kutapatapa. Na maneno kama hayo ameshazowea kuyasema mara nyingi tangu alivyofukuzwa CCM,” alisema Nape.

SOKO LA MAHINDI
Alisema kamati kuu pia ilijadili suala la soko la mahindi na kuiagiza serikali kuangalia upya mfumo unaotumiwa na Hifadhi ya Taifa ya Chakula (NFRA) katika ununuzi wa zao hilo.

Nape alisema utaratibu wa sasa, ambao kwa kiasi kikubwa unanufaisha zaidi mawakala badala ya wakulima moja kwa moja, unatakiwa ubadilishwe ili uwanufaishe zaidi wakulima.
CHANZO: NIPASHE
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa