Home » » KUNA TOFAUTI YA MAABARA NA MAJENGO YA MAABARA

KUNA TOFAUTI YA MAABARA NA MAJENGO YA MAABARA

  Mwenyekiti wa Halimashauri ya Musoma vijijini ambae ni Diwani wa Kata ya Nyankanga Magina Magesa,  akikagua ujenzi wa maabara katika shule ya sekondari Bisumwa, juzi
Desemba 9 mwaka jana ndiyo ulikuwa mwisho wa utekelezaji wa agizo la Rais Jakaya Kikwete kuhusu ujenzi wa maabara katika shule za sekondari za Serikali nchi nzima.
Akiwa katika mikutano ya hadhara katika Wilaya za Lushoto na Kilindi mkoani Tanga Julai, Rais Kikwete aliagiza ifikapo Novemba 30 aone vyumba vya maabara vimekamilika. Kutoka Novemba 30 muda ukaongezwa hadi Desemba 9.
Utekelezaji wa ujenzi
Tayari kuna mikoa iliyotekeleza ujenzi huo kwa asilimia zaidi ya 90, mingine asilimia 50 na hata 30 kwa baadhi ya mikoa.
Mikoa iliyotekeleza agizo hilo na asilimia katika mabano ni Dar es Salaam (100), Mbeya (95.45), Njombe (95), Kigoma chini ya asilimia 40, Morogoro (60) na Ruvuma zaidi ya asilimia 92.
Katika maeneo mengi utekelezaji wa ujenzi huu umekumbwa na kadhia nyingi zikiwamo walimu kukatwa fedha kwa nguvu, wananchi kutishwa na hata baadhi ya watendaji kuvuliwa nyadhifa zao na wengine kukumbana na kipigo.
Mfano barua ya Septemba 15, mwaka 2014 kutoka Halmashauri ya Kongwa mjini Dodoma kwenda kwa waratibu wa elimu wa kata, iliwataka watendaji hao kuhakikisha wanakusanya fedha za michango kutoka kwa walimu.
Barua hiyo ilibainisha viwango vilivyotakiwa kutolewa ku ni Sh60,000 (waratibu elimu kata), Sh60,000 (walimu ngazi ya mshahara TGTS F-G), Sh30,000 (ngazi ya mshahara TGTS D-E) na Sh20,000 (TGTS B-C).
Mratibu wa Mtandao wa Elimu Tanzania (TenMet), Cathleen Sekwao, anasema huwezi kuwaeleza wananchi wachangie maabara wakati wanaona fedha zipo ila wanafaidi wachache.
“Watu wanachota pesa wanakula halafu unapofika wakati wa uboreshaji wa elimu wananchi wachangie, kweli hiyo Sh1.6 trilioni si ingetosha kujenga hizo maabara lakini je, waliokula wamechukuliwa hatua gani,” anasema na kuongeza:
“Fedha zipo na wananchi, walimu wanalia kuchangishwa, mifumo ya uongozi ni mibovu kwani ingekuwa imara rasilimali tulizonazo zinazopotea kwa wajanja kujinufaisha wao ndiyo inatufikisha hapa.’’
Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba katika mahojiano na gazeti hili Oktoba mwaka jana, alikaririwa akisema Serikali imekuwa ikipoteza zaidi ya Sh1.6 trilioni kwa mishahara hewa nchini kila mwaka.
“Ukisoma taarifa za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), utagundua zaidi ya Sh1.6 trilioni zinapotea kutokana na mishahara hewa, fedha inayotosha bajeti ya wizara,” alieleza Nchemba.
Kwa wadau wengi wa elimu, fedha anazotaja Mwigulu na nyinginezo zingeweza kutumika katika vipaumbele ikiwamo ujenzi huo wa maabara ambao sasa unaendeshwa kwa nguvu ya wananchi kupitia maagizo ya viongozi wa Serikali.
Fedha nyingine zinazoweza kutumika katika shughuli za maendeleo ni pamoja na zile zinazosamehewa katika misamaha ya kodi. Kwa mfano Bajeti ya Serikali ya mwaka 2013/14, inaonyesha kwa mwaka huo zaidi ya Sh1.6 trilioni zilipotea kupitia misamaha ya kodi.
Walimu wa Sayansi
Wakati hamasa ya sasa ikiwa ni ujenzi wa maabara, baadhi ya watu wanauliza kuna mikakati gani ya kuwapata wataalamu wa maabara hizo na hata vifaa husika?
Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Ezekiel Oluoch anasema katika masomo ya Fizikia, Kemia na Baiolojia kuna upungufu wa asilimia 50 ya walimu.
Anasema jumla ya shule za sekondari za kata nchi nzima ziko 3,500 na zote hazina maabara na kwa maabara za masomo ya sayansi inahitaji wataalamu wa maabara mmoja, hivyo kwa zote watahitajika watatu.
“Kwa idadi hiyo jumla ya wataalamu wa maabara 12,000 watahitajika…maabara zinatakiwa kuwa zimekamilika Novemba 30 mwaka huu je, walimu wa kuziendesha wanatoka wapi au tutakuwa na majengo tu ya maabara?’’ anasema.
Anaongeza: “Nilichokuwa nakiona mimi wakati Serikali inapanga kujenga maabara, ingepanga pia kuandaa walimu wa kutosha na wataalamu wa maabara hizo lakini sasa tujiandae kuwa na majengo ya maabara na si maabara kama wanavyodai.”
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Dk Romanus Dimoso anasema changamoto anayoitazama katika ujenzi wa maabara ni ndogo kuliko ujenzi huo utakapokamilika.
“Sitoshangaa kama nikiona au kusikia majengo hayo yamebadilishwa matumizi kwani gharama za ujenzi kama tunahangaika hivi itakuaje gharamza za vifaa vya kufundishia na kujifunza ambavyo ni kubwa kuliko ujenzi wenyewe?” anahoji.
“Walimu bado ni tatizo na hata waliopo hawakusoma kwa vitendo na walijikita kinadharia zaidi sasa unapotaka watumike katika maabara sijui itakuaje,” anaongeza kusema.
Kauli ya Wizara
Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, (Tamisemi) anayeshughulikia elimu, Kassimu Majaliwa anasema maabara zitakapokamilika watawasiliana na ofisi ya utumishi ili kuhakikisha wataalamu wanaajiriwa.
“Mbali na walimu pia tutafanya juhudi za kuwaajiri wataalamu wa maabara hizo ambao watakuwepo katika maabara hizo ili kurahisisha zoezi zima la utoaji wa huduma kwa wanafunzi,” anasema.
 Chanzo:Mwananchi

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa