Home » » Kampuni kufundisha wakulima 100,000 shamba darasa

Kampuni kufundisha wakulima 100,000 shamba darasa


Mwandishi Wetu, Songea
KAMPUNI ya Lutukira Mixed Farm Project  yenye makao yake jijini  Dar es Salaam imepanga kutoa mafunzo ya shamba darasa kwa wakulima 100,000 watakaozunguka eneo la mradi wa  uwekezaji wa kilimo  cha karanga,ufuta  na alizeti  wilayani Songea.

Mradi huo tayari umepata eneo la ekari 20,000 za kulima mazao ya kibiashara na kujenga kiwanda cha kukamua mafuta ya mbegu. Wakulima watakaofundishwa watalima mazao mbalimbali na kuyauza kwenye kampuni hiyo ambayo itayakamua na kuyaunza nje ya nchi. 

Mwenyekiti ambaye pia ni  Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni  hiyo, Alhaji Said Kilahama alisema hayo jana jijini hapa alipozungumzia mkakati ya kutekeleza mradi wa kilimo Lutukira Mixed Farm Project.
Alisema  mafunzo hayo yatatolewa katika kipindi cha miaka 10 ijayo  kwa njia ya vitendo.

Kilahama alisema kampuni yake itatekeleza mpango huo katika Kijiji cha Lutukira ambako  imepata ekari 50,000 za mradi wa kilimo cha kibiashara kwa  mazao ya karanga, ufuta  na alizeti na kwamba kwa sasa tayari ekari 300 zimelimwa.

“Ndugu waandishi, kampuni yangu kwa ushirikiano na Kampuni ya Montara Land Limited iliyoandikishwa Seychelles ilianza  mradi kwa kutenga Dola 3 milioni za Marekani  ili kupata eneo la kilimo cha kibiashara ikiwa ni kuitikia wito wa Serikali ya Tanzania kuboresha kilimo nchini’’ alisema.

Alisema mradi huo utaajiri  wafanyakazi  61 wa kudumu na wengine 100 watakuwa wakiajiriwa wakati wa kipindi maalumu cha kazi nyingi.

Mwenyekiti huyo alipongeza ushirikiano mzuri alioanza kuupata kutoka kwa wananchi  wa Lutukira ,viongozi wa Wilaya ya Songea na Mkoa wa Ruvuma  kwa ujumla katka kutekeleza mpango huo.

Kuhusu huduma za jamii, Kilahama alisema mradi huo utashirikiana kwa karibu na wananchi ambapo  sasa inawapatia trekta wananchi ili walitumie katika kilimo na kwamba pia itashirikiana na  Serikali katika kupunguza kero za jamii hususan masuala ya afya, elimu, maji  na kuondoa njaa nchini.

Aliwataka wakazi wa Mkoa wa Ruvuma kwa ujumla kutoa ushirikiano kwa kulima mazao ya alizeti na karanga ambayo yatakuwa na soko la uhakika katika kampuni yake.Hivi karibuni Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma ,Said Mwambungu alinukuliwa akiwataka wakazi wa mkoa huo kushirikiana vizuri na wawekezaji.
Chanzo: Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa