Home » » Wafanyabiashara Songea walazimishwa kugoma

Wafanyabiashara Songea walazimishwa kugoma

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Baadhi ya wafanyabiashara wa mjini Songea wamelazimishwa na wenzao kuingia katika mgomo wa kupinga matumizi ya mashine za kielektroniki za kutolea risiti za EFD.
Waliolazimishwa ni wamiliki wa baa na vituo vya kuuza mafuta ambao wamekuwa wakiendelea kufanya biashara zao kabla ya baadhi ya wenzao kukodisha ‘mabaunsa’ kuwalazimisha kufunga biashara zao kwa kile kilichoelezwa kuwa ni wasaliti.
Pamoja na serikali mkoani Ruvuma kutumia polisi kufanya doria katika maeneo mbalimbali ya mji mgomo huo umeendelea huku wahusika wakishinikiza Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Mkoa wa Ruvuma, Apily Mbaruku afukuzwe kazi au ache kuwaandikia barua za vitisho za kutumia mashine hizo.
Akizungumzia shinikizo hilo, Mbaruku alisema hatishwi na wafanyabiashara hao na kusema kuwa TRA inawataka wafanyabiashara kuendelea kutumia mashine hizo.
Akizungumza wakati wa kikao kilichofanyika kwenye Ukumbi wa Bombambili jana, msemaji wa wafanyabiashara hao, John Oscar alisema wamechoka kuburuzwa na TRA na safari hii mgomo walioitisha ni mkubwa ukihusisha wafanyabiashara wa kada mbalimbali.
Alidai kuwa mashine hizo ni mpango wa wakubwa ambao wanataka kupata fedha kupitia wao na kumtaka meneja wa TRA wa mkoa kuacha tabia ya kuwakejeli kuwa hawana uwezo wa kufunga maduka kwa wiki moja.
Akisoma maazimio ya mkutano huo, makamu mwenyekiti wa umoja wa wafanyabiashara hao, Wilson Mbilinyi alisema hawatafungua maduka yao kwa siku mbili na baada ya hapo wataandamana kwenda ofisi za TRA kwa ajili ya kuzifunga kutokana na kushindwa kusikiliza matatizo yao.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa