Home » » MWAMBUNGU AMPONGEZA MKANDARASI

MWAMBUNGU AMPONGEZA MKANDARASI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
MKUU wa Mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu, amepongeza mradi wa ujenzi wa majengo ya Shule ya Sekondari Unberkant iliyopo kwenye Kata ya Mtipwili wilayani Nyasa mkoani hapa unaofanywa na Kampuni ya Ovans Construction (Ltd) ya Mbinga.
Mradi huo unafadhiliwa na Benki ya Dunia (WB) kupitia Serikali ya Tanzania kwa thamani ya sh 288,254,380.
Mwambungu alitoa pongezi hizo mwishoni mwa wiki baada ya kutembelea shuleni hapo kwa lengo la kujionea maendeleo ya ujenzi alipofanya ziara wilayani Nyasa.
Alisema mkandarasi anayesimamia mradi huo anastahili pongezi kwa kuonyesha uzalendo na uaminifu katika ujenzi huo wa kiwango kinachotakiwa ambapo amewataka wengine kuiga mfano huo kwa madai kwamba hali hiyo itasaidia kuokoa fedha nyingi za serikali ambazo zinapotea kutokana na baadhi yao kujenga miradi chini ya kiwango.
Kutokana na hali hiyo mkuu wa mkoa huyo amezitaka halmashauri zote mkoani hapa kuhakikisha zinatoa kazi za ujenzi kwa makandarasi wazalendo, huku akionya matendo ya rushwa kwa madai kwamba kufanya hivyo kunasababisha kupata makandarasi wabovu.
Kwa upande wake, mkuu wa shule hiyo ya sekondari, David Kilowoko, akisoma taarifa ya shule yake mbele ya mkuu wa mkoa huyo, alisema mradi huo wa ujenzi wa nyumba moja ya mwalimu, maabara moja, matundu nane ya vyoo vya wanafunzi, mfumo wa uwekaji wa umeme wa jua na mfumo wa maji ya kisima na ukarabati wa vyumba sita vya madarasa umefanikiwa kupitia mpango wa matokeo makubwa sasa unaotekelezwa katika sekta ya elimu.
Kilowoko alisema kupitia Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari wa awamu  ya pili (SEDP II), shule hiyo pia imepata kiasi cha shilingi milioni 26 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba moja ya mwalimu ambayo itatumiwa na familia za walimu wawili.
Akizungumzia kwa upande wa taaluma, alisema kuwa shule hiyo inakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa walimu wa masomo ya sayansi ambapo hadi sasa shule hiyo ina mwalimu mmoja tu wa somo hilo na kudai kwamba hali hiyo imesababisha kupata matokeo yasiyoridhisha ambayo yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na upungufu wa walimu.
Aidha mkuu huyo wa shule ameishukuru serikali kwa jitihada zake za kuboresha miundombinu ya shule jambo ambalo amedai kuwa hali hiyo itakuwa chachu ya maendeleo ya elimu kutokana na kuwa mazingira ya kusomea na kufundishia yatakuwa rafiki.
Chanzo;anzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa