Home » » JK AWAHAKIKISHIA WAKULIMA BEI YA MAHINDI 500/-KWA KILO

JK AWAHAKIKISHIA WAKULIMA BEI YA MAHINDI 500/-KWA KILO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Rais Jakaya Kikwete
Rais Jakaya Kikwete amewahakikishia wakulima wa zao la mahindi mkoani Ruvuma  kuwa serikali itanunua mahindi yote kwa Sh. 500 kwa kilo badala ya Sh. 450.
Alisema hayo wakati akihutubia mamia ya wakazi wa manispaa ya Songea kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa michezo wa Majimaji mjini hapa.

Alisema kuwa mkoa wa Ruvuma ni miongoni mwa mikoa saba inayoongoza kwa kilimo cha zao la mahindi hivyo serikali lazima iwaunge mkono kwa kuhakikisha kuwa mahindi yote yaliyolimwa katika msimu wa mwaka huu yananunuliwa yote na fedha ya kununulia mahindi hayo lazima itapatikana.

Alisema kwa vile kwenye Ghala la Hifadhi la chakula la Taifa (NFRA) mkoani Ruvuma mahindi yamefurika, ni lazima magari ya jeshi yatumike kusafirisha mazao ili kuhakikisha kuwa yanatolewa kwenye ghala kuu na kupata nafasi ya kupokea mahindi mapya yatakayoanza kununuliwa katika msimu unaotarajiwa kuanza Agosti mosi, mwaka huu.

“Ndugu wananchi dhamira yangu ya kufanya ziara katika mkoa wenu ni kutaka kukagua shughuli mbalimbali za maendeleo na kuwahamasisha wananchi kufanya kazi kwa bidii ili kusukuma gurudumu la Taifa.”alisema Kikwete.

Alisema kuwa amefurahishwa na kazi iliyofanywa na wakulima pamoja na NFRA  kwa kununua na kuhifadhi mahindi vizuri na kuondoa hofu ya  kuwapo njaa Tanzania.

Akizungumzia ujenzi wa barabara za manispaa kwa kiwango cha rami, Rais Kikwete alimuagiza Waziri wa Miundombinu Dk. John Magufuli kuhakikisha barabara ya kutoka Songea Girls hadi njia panda ya Ndilimalitembo inajengwa kwa kiwango cha lami kufikia mwakani.

Aidha amemuagiza Mkuu wa Mkoa huo, wakuu wa wilaya, wakurugenzi wa halmashauri za wilaya na manispaa pamoja na wenyeviti wa Halmashauri kuhakikisha kuwa shule zote za sekondari za serikali zinakuwa na maabara ili kuongeza idadi kubwa ya wanafunzi wa masomo ya sayansi .

Rais Kikwete alizindua ghala jipya la wakala wa  NFRA lenye uwezo wa kuhifadhi tani 5000, mradi wa nyumba 18 za bei nafuu za Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) pamoja na  ofisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).
 
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa