Home » » Wanafunzi wamtaka mkuu wa chuo cha ualimu aachie ngazi

Wanafunzi wamtaka mkuu wa chuo cha ualimu aachie ngazi



WAKUFUNZI na wafanyakazi wa Chuo cha Ualimu Songea, wameilalamikia Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kwa kitendo cha kushindwa kushughulikia mgogoro uliopo chuoni hapo na kusababisha shughuli mbalimbali za kiutendaji kudorora.
Kutokana na hali hiyo, wanafunzi hao wameelezea hofu ya kutofanikisha mpango mkakati wa serikali wa Matokeo Makubwa Sasa na kuitaka serikali kumuondoa madarakani Mkuu wa Chuo hicho, Ubaya Suleiman, ili kukinusuru chuo hicho.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti jana, viongozi wa wanafunzi hao ambao waliomba majina yao yahifadhiwe, walisema kuwa katika chuo hicho kuna mgogoro ambao umeshindwa kuchukuliwa hatua na kusababisha amani na utulivu kukosekana chuoni hapo kwa zaidi ya miezi saba sasa.
Walisema kuwa mgogoro huo umetokana na uongozi mbovu usiozingatia misingi ya uongozi na demokrasia katika vyuo vya ualimu nchini kwani mkuu wa chuo hicho, amekuwa mbabe, lugha chafu na mtu wa vitisho kwa wafanyakazi na wanachuo.
“Pamoja na hayo, mkuu huyo wa chuo amediriki kuwapeleka baadhi ya wafanyakazi wake kwenye vyombo vya dola (polisi), akiwatuhumu kuwa wanataka kumuua.
“Baada ya mgogoro huo kutopata suluhu kupitia vikao vya ndani, jitihada zifuatazo zilifanyika na wafanyakazi wa chuo hicho ili kuleta hali ya amani na utulivu.”
Walifafanua kuwa Aprili 27 mwaka huu, walifanya kikao na mkuu wa wilaya ya Songea Joseph Mkirikiti, Mei 15 na Juni mosi mwaka huu, walifanya kikao na bodi ya ushauri ya chuo, hata hivyo suluhu ya mgogoro huo haikupatikana.
Walisema kuwa kutokana na hali hiyo, Katibu Mkuu Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Profesa Sifuni Mchome aliunda tume ya watu watano ikiongozwa na mkaguzi mkuu wa shule na vyuo wa nyanda za juu kusini ambaye alifahamika kwa jina moja la Lyapambile, kuja kufanya utafiti wa chanzo cha mgogoro, lakini mpaka sasa tume hiyo haijatoa majibu ya uchunguzi wa jambo hilo.
“Hata hivyo wakufunzi hawakuishia hapo Agosti 13, 2013 walifanya kikao na Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Saidi Mwambungu, ambaye baada ya kusikiliza mgogoro huo aliahidi kuleta suluhisho la kudumu mapema iwezekanavyo ili kuleta amani na utulivu chuoni hapo. Lakini cha kushangaza hadi sasa yapata miezi mitatu hakuna kilichofanyika hali ambayo imeendelea kuwavunja moyo wafanyakazi wa chuo hicho,” walisema.
Mkuu wa chuo hicho, Ubaya Suleiman, alipoulizwa kuhusu mgogoro huo, alisema hana jambo la kuzungumza kwani mgogoro huo uko kwenye Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi hivyo hawezi kusema chochote.
Kwa upande wake Kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo ambaye amejitambulisha kwa jina la H. Lugome ameonyesha masikitiko makubwa sana juu ya utendaji wa mkuu wa chuo hicho na kuahidi kukutana na wafanyakazi hao ili kuweza kufanya kikao cha mwisho cha majadiliano.
Naye Naibu Waziri wa Elimu Philipo Mulugo alipotafutwa kupitia simu yake ya kiganjani, alisema swala hilo bado halijafika mezani kwake na endapo likifika basi atachukua hatua stahiki 

Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa