Home » » DC AOMBWA KUINGILIA MZOZO WA ARDHI

DC AOMBWA KUINGILIA MZOZO WA ARDHI

na Julius Konala, Mbinga
UONGOZI wa Shule ya Sekondari Agustino iliyoko katika wilaya ya Mbinga, mkoani Ruvuma, umemuomba mkuu wa wilaya (DC) hiyo, Senyi Ngaga, kuingilia kati kutatua mgogoro wa ardhi baina yao na wananchi wenye mashamba yanayozunguka eneo la shule hiyo.
Ombi hilo lilitolewa jana na mkuu wa shule, Moses Mapunda kwa mkuu wa wilaya hiyo wakati akitoa taarifa ya shule yake katika mahafali ya kwanza ya kidato cha nne yaliyofanyika shuleni hapo.
Mapunda alisema mpango wa shule hiyo ni kuendeleza upanuzi na kujenga chuo cha ualimu kwa ngazi ya cheti na stashahada, lakini juhudi hizo zinapingwa na wananchi wenye mashamba yanayozunguka eneo hilo kwa kutaka fidia kubwa ya sh milioni sita kwa shamba la nusu hekari lisilo na zao lolote.
Alisema kuwa serikali imeshayatenga maeneo hayo kisheria kwa ajili ya matumizi ya ujenzi wa taasisi za elimu pamoja na viwanja vya michezo na sio kwa matumizi ya kilimo au makazi, jambo ambalo amemuomba DC Ngaga kushirikisha wahusika wa Idara ya Ardhi pamoja na mthaminishaji wa ardhi wa serikali ili aweze kufanya tathmini ya mashamba hayo kwani mkurugenzi wa shule hiyo yuko tayari kulipa fidia halali.
Mbali na suala hilo, aliiomba serikali kuangalia uwezekano wa kuzisaidia vifaa vya maabara, vitabu na fedha shule za watu binafsi pindi inapopata msaada toka nje badala ya kuelekeza nguvu kwenye shule za serikali pekee kwani zote zinatoa mchango mkubwa wa elimu kwa Watanzania.
Akizungumzia kwa upande wa taaluma alisema shule yake imeweza kufanya vizuri ambapo mwaka 2009 shule hiyo ilishika nafasi ya kwanza kati ya shule zote zilizofanya mitihani ya wilaya kwa kidato cha kwanza ambapo kati ya wanafunzi kumi bora walitoa wanafunzi saba.
Alisema mwaka 2010 shule ilishika nafasi ya kwanza katika mitihani ya kidato cha pili kwa mkoa ambapo ilishika nafasi ya 46 kati ya shule 387 za Kanda ya Nyanda za Juu Kusini ambapo wanafunzi wote 70 waliofanya mitihani hiyo walifaulu.
Aliongeza kuwa katika matokeo ya mitihani ya taifa ya kidato cha sita mwaka 2011, walishika nafasi ya pili kati ya shule sita kimkoa na ya 32 kati ya 129 kitaifa kwa shule zenye watahiniwa chini ya 30 na kwamba wanafunzi 11 walifaulu na kuendelea na masomo ya elimu ya juu.
Alizitaja changamoto zinazoikabili shule hiyo kuwa ni pamoja na upungufu wa vitabu vya kiada na ziada, vifaa vya maabara na udogo wa eneo la shule na ukosefu wa viwanja kwa ajili ya kufanyia michezo ya wanafunzi, huku akipongeza jitihada zinazofanywa na serikali katika kusogeza huduma ya nishati ya umeme jambo ambalo litawezesha wanafunzi kujifunza masomo ya kompyuta na kujisomea usiku.
Kwa upande wake DC Ngaga alisema kuwa serikali kwa muda mrefu imekuwa ikithamini michango inayotolewa na sekta binafsi katika suala la elimu na kwamba itaendelea kutoa ushirikiano katika hilo kwa kuweka mazingira mazuri.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa