Home » » DC MSTAAFU ADAI KUTELEKEZWA

DC MSTAAFU ADAI KUTELEKEZWA

na Julius Konala, Songea
SERIKALI imedaiwa kumtelekeza bila matibabu mpigania uhuru ambaye amewahi kuwa mkuu wa wilaya kadhaa nchini, Josephat Mhagama (75), maarufu kama (Lilikuliku) aliyelazwa katika Hospitali ya Mkoa wa Ruvuma sasa.
Akizungumza na waandishi wa habari hospitalini hapo, mkewe, Eva Komba, alisema kuwa Mhagama alilazwa zaidi ya mwaka mmoja bila msaada wowote toka serikalini na kwamba hakuna kiongozi yeyote aliyewahi kumtembelea.
Eva ambaye alisoma darasa moja na Spika wa Bunge, Anne Makinda, katika Shule ya Kati Peramiho, alisema mumewe anasumbuliwa na maradhi mbalimbali yakiwemo matatizo ya kibofu cha mkojo, kwikwi na uti wa mgongo hali inayomfanya alale muda mrefu.
Alifafanua kuwa Mhagama alizaliwa mwaka 1937 katika kijiji cha Njoomlole, wilayani Namtumbo, na kusoma shule ya kati Peramiho kisha Sekondari ya Kigonsera ambapo alikutana na Rais mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa, ambaye alimtangulia darasa moja mbele.
Alisema kuwa baada ya kumaliza masomo yake aliajiriwa kama bwana shamba wa wilaya ya Songea na kuamua kuacha kazi baada ya kutofautiana na serikali ya kikoloni wakati huo kwa vile alitaka usawa kati ya Wazungu na Waafrika ambapo alirudi kijijini Njoomlole na kuwa Katibu wa TANU wa tawi.
“Mwaka 1963 hadi mwaka 1970 mume wangu alikuwa Katibu Mtendaji wa TANU wa Wilaya ya Songea na mwaka 1965 akagombea ubunge katika jimbo la Songea Kaskazini akichuana na Otien Kambona na kumshinda,” alisema Eva.
Aliongeza kuwa mumewe huyo mwaka 1970 aliteuliwa kuwa Katibu wa TANU wa Mkoa wa Dodoma na mwaka 1971 alipelekwa Singida ambako alifanya kazi na hayati Moses Nnauye ambaye wakati huo alikuwa mkuu wa mkoa huo na baadaye alifanya kazi na Kingunge Ngombale Mwiru.
“Baadaye walihamishiwa Tanga wakati yeye akiwa Katibu wa TANU, Kingunge alikuwa Mkuu wa Mkoa na Oktoba 1975 aliteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Karagwe mkoani Kagera, mwaka 1976 akahamishiwa wilayani Biharamulo hadi mwaka 1980 alipohamia Muheza,” alisema.
Eva aliongeza kuwa mwaka 1981 mumewe alihamishiwa wilayani Manyoni hadi mwaka 1983 aliporejeshwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Songea na mwishoni mwaka huo akastaafu na kurudi kijijini kwake Njoomlole.
Chanzo: Tanania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Ruvuma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa